SONIA Mgogo, Mbunge wa Viti Maalum (CUF), ameitaka serikali kueleza mpango wake wa kuwawezesha madaktari bingwa ili wafanye kazi nchini. Anaripoti Danson Kaijage, Ddodoma … (endelea).
Mbunge huyo ameuliza swali la nyongeza leo tarehe 3 Septemba 2019 kwamba, asilimia kubwa ya wananchi wana kipato cha chini na wamekuwa wakitegemea hospitali za serikali, je serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha madaktari bingwa wachache waliopo, hawapati vishawishi vya kufanya kazi nje ya nchi au katika hospitali binafsi?.
Pia ametaka kujua kama serikali imejipanga kuhakikisha inaongeza madaktari bingwa na kuwagawa kwa uwiano ili kusaidi kuwapunguzia gharama za huduma za afya nje ya nchi.
Awali, katika swali la msingi mbunge huyo alitaka kujua, serikali ina mkakati gani wa kuongeza madaktari bingwa nchini?
Dk.Faustine Ndugulile, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto amesema, licha ya kuwa madakitari bingwa ni wachache lakini bado wanaboreshewa mazingira ya kufanyia kazi.
Amesema, serikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha inapanga madaktari bingwa kwa uwiano ambao unaonekana kuwa na tija, ili kuondokana na changamoto mbalimbali za uhaba wa madaktari bingwa.
Pia Dk. Ndugulile amesema, serikali inaendelea kuimarisha huduma za kibingwa katika ngazi mbalimbali za huduma nchini ikiwa ni pamoja na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).
Amesema, katika mwaka wa fedha 2017/18, wizara kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ilitenga kiasi cha Sh. 2 Bil zilizotumika kwa ajili ya kusomesha madaktari bingwa 125 wa fani za kipaumbele katika Chuo cha MUHAS ambao wanatarajiwa kumaliza 2020/2021.
Na kuwa, katika mwaka wa fedha 2018/19 serikali ilitenga kiasi cha Sh. 18 Bil ili kuendelea kugharamia mafunzo ya ngazi ya kibingwa katika kada mbalimbali za afya 127 katika Chuo cha MUHAS.
Leave a comment