MBUNGE wa Chilonwa, Joel Makanyaga (CCM) ameshangazwa na Serikali kutoruhusu wananchi kujenga shule wenyewe hata madarasa mawili kila mwaka ili kupunguza masangamano wa wanafundi madarasani. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Mbunge huyo amesema, shule nyingi za msingi nchini Tanzania zina wanafunzi wengi wanaozidi kiwango kinachotakiwa cha wanafunzi takribani 700.
Kutokana na hali hiyo, mbunge huyo alisema ni kwa nini, Serikali isiruhusu wananchi wajenge shule nyingine kwa mpango wa kujenga hata madarasa mawili kila mwaka na shule hizo zikatambuliwa kisheria.
Akijibu swali hilo, Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais – Tamisemi amesema, wananchi wanaruhusiwa kujenga shule katika maeneo yenye mahitaji kwa kushirisha viongozi wa Halmashauri ili kusogeza huduma karibu na wananchi.
Amesema kupitia utaratibu huo, Serikali imefanikiwa kuwa na shule ya msingi kila Kijiji na Shule za Sekondari kila Kata.
Aidha, amesema, Serikali kwa kushirikisha nguvu za wananchi imekuwa na utaratibu wa kujenga vituo shikizi katika maeneo ambayo shule mama iko mbali ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.
Amesema, serikali kutokana na kuwepo kwa vituo hivyo, baadhi ya vituo hivyo baadaye husajiliwa kuwa shule baada ya kukidhi vigezo vinavyotakiwa.
Leave a comment