MBUNGE wa Kigoma Kaskazini (CCM), Assa Makanika, ameiomba Serikali ya Tanzania, kuwasaidia wananchi wa jimbo hilo, ambao wamekuwa wakikamatwa kwa kuitwa wakimbizi ili waweze kuishi kwa amani katika mkoa wao. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Ombi hilo limetolewa leo Ijumaa, tarehe 4 Juni 2021, bungeni jijini Dodoma, wakati wa kipindi cha maswali na majibu.
Mbunge huyo amesema, wananchi wa mkoa huo, wamekuwa wakipata tabu za kukamatwa mara kwa mara kwa kuitwa wakimbizi hali inayosababisha kukosa amani.
“Je, ni lini serikali itawasaidia wananchi wa kigoma ambao wamekuwa wakikamatwa mara kwa mara kwa kuitwa wakimbizi nchini mwao,” amehoji Makanika.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, Khamis Chilo amesema, wizara hiyo kupitia Idara ya Uhamiaji, imepewa jukumu la kudhibiti, kusimamia na kufuatilia uingiaji, ukaaji na utoaji wa wageni hapa nchini.
Chilo amesema, katika kutimiza jukumu hilo, Idara ya Uhamiaji imekuwa ikifanya operesheni, doria na misako mbalimbali kwa lengo la kubaini wageni wanaoingia na kuishi nchini kinyume cha sheria na taratibu.
“Serikali imekuwa ikifanya mahojiano na uchunguzi wa kina ili kujiridhisha juu ya uraia wa watuhumiwa wanaokamatwa wakati wa operesheni husika.”
“Idara ya Uhamiaji, katika kushughulikia masuala ya uraia, huzingatia matakwa ya sheria ya uraia sura 357 rejeo la mwaka 2002, Operesheni, doria na misako hufanyika kwa mikoa yote na si mkoa wa kigoma pekee,” amesema Chilo.
Katika swali la nyongeza, liliulizwa kwamba kiwango cha usumbufu kinachofanywa kinavuka mipaka “na tunaomba waziri atueleze kwa nini misako na doria imekuwa mingi na kuzua usumbufu kwa wananchi.”
Akijibu swali hilo, Waziri wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene alisema, doria hiyo inafanyika nchi nzima na si Kigoma pekee na kuhusu vitambulisho vya Taifa (NIDA), vinatolewa hata kwa wakazi ambao si raia “na si kwamba ukipewa kitambulisho, hutoulizwa tena, hapana, utaulizwa sehemu yoyote.”
Leave a comment