MBUNGE wa Mbogwe mkoani Geita (CCM), Henry Maganga, ameiomba Serikali iwafutie madeni wafanyabiashara, wenye madeni yanayotokana na ukosefu wa elimu juu ya matumizi sahihi ya Mashine za Risiti za Kielektroniki (EFD). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Maganga ametoa ombi hilo leo Ijumaa tarehe 21 Mei 2021, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini Dodoma.
“Bado wafanyabiashara wana kilio hapa nchini, hawana furaha na Serikali yao. Hawakuwa na elimu juu ya mashine ya EFD, naomba Serikali itoe kauli ili nchi ijue wamesha samehewa madeni,” amesema Maganga.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhandisi Hamad Masauni, amesema Serikali itafanya tathimini juu ya maombi hayo, ili kujua faida na athari zake, endapo itasamehe madeni hayo.
“Kauli ya Serikali kuhusu kusamehe madeni haiwezi kutolewa kwa utaratibu huu, msamaha wa madeni uko kwa mujibu wa sheria . Kwa hiyo hatuwezi kusimama hapa tukatoa tamko kusema tunamsamehe nani madeni,” amesema Mhandisi Masauni na kuongeza:
“Ili msamaha utoke lazima tukae chini kufanya tahimini na utafiti wa kina, kuona athari na faida za kufanya hivyo.”
Leave a comment