MBUNGE wa Mtambile, Masoud Abdallah Saim (CUF) ameihijo serikali ina mipango gani ya kupiga marufuku tabia ya watu kurithi wajane, anaandika Dany Tibason.
Mbunge huyo alitoa hoja hiyo jana bungeni alipokuwa akiuliza swali la nyongeza kwa kutaka kujua ni hatua gani serikali inachukua kukomesha vitendo vya ndoa za kurithisha wanawake jambo ambalo linaweza kusababisha ongezeko la maambukizi ya magonjwa.
Awali katika swali la msingi la mbunge wa Lupembe, Joramu Hongali (CCM) alitaka kujua ni lini serikali itaongeza bajeti ya ujenzi, vifaa tiba na madawa katika kila kijiji na vituo vya afya kila kata.
“Waathirika wa Ukimwi katika halmashauri ya wilaya ya Njombe wamekuwa wakipoteza maisha haraka zaidi kutokana na kutembea umbali mrefu kwenda kupata huduma za matibabu.
“Je nilini Serikali itaongeza Bajeti ya ujenzi, vifaa tiba katika kila kijiji na vituo vya Afya kwa kila kata,” alihoji Hongoli.
Akijibu maswali hayo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Seleman Jafo amesema serikali inaendelea kupiga vita suala la kuwepo kwa ndoa za kurithishana.
Jafo amesema halmashauri ya wilaya ya Njombe ilitengewa bajeti ya Sh. 295 milioni kwa mwaka wa fedha 2016/17 tayari Sh. 87 milioni zilipelekwa na kuelekezwa katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya Afya.
Alieleza kuwa kwa mwaka wa fedha 2017/18 halmashauri hiyo imetengewa bajeti ya Sh. 435 milioni sawa na ongezeko la asilimia 47.
Aidha amesema kuwa serikali imeongeza fedha za mfuko wa pamoja kutoka Sh. 259 milioni zilizotengwa mwaka wa fedha 2016/17 hadi Sh. 306.2 milioni kwa mwaka wa fedha sawa na ongezeko la asilimia 18.
Leave a comment