GRACE Tendega, Mbunge viti maalumu (asiye na chama), ameitaka serikali ya Tanzania, kuona umuhimu wa huduma za afya kwa wazee, watoto na wajawazito. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea)
Ameyasema hayo leo Jumatano, tarehe 19 Mei 2021, katika kipindi cha maswali na majibu bungeni jijini Dodoma.
Tendega amesema, kumekuwa na changamoto ya huduma za afya katika Zahanati zetu hasa ukosefu wa dawa pamoja na ukosefu wa huduma bure kwa wazee, watoto na akinamama wajawazito.
“Je, ni lini Serikali itahakikisha sera ya afya inatekelezwa bila tatizo lolote?”
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Tamisemi, David Silinde amesema, katika kuhakikisha inaboresha upatikanaji wa dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini, Serikali imeongeza bajeti ya bidhaa za afya kutoka Sh.31 bilioni katika mwaka wa fedha 2015/16 hadi Sh. 270 bilioni.
“Katika mwaka wa fedha 2020/21, ongezeko hilo la bajeti na fedha, inayotolewa limesababisha hali ya upatikanaji wa dawa za msingi (tracer medicine) kuongezeka kutoka wastani wa asilimia 35 hadi asilimia 90,” amesema Silinde.
Pia, kuna changamoto ya upatikanaji wa dawa za makundi maalum nje ya dawa za msingi (tracer medicine) hasa katika ngazi ya Zahanati ambapo dawa nyingi zinazohusu magonjwa ya uzeeni zinaangukia kwenye kundi hilo.
“Ili kukabiliana na changamoto hiyo, Mei 2021 Serikali imeipatia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wazee na Watoto Sh.80 bilioni kwa ajili ya kununua dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ya msingi, dawa zitakazo nunuliwa zitapunguza tatizo la dawa kwa kiasi kikubwa,”
“Serikali inaendelea kudhibiti mianya ya upotevu wa dawa ili kuhakikisha kuwa dawa zinazonunuliwa zinawanufaisha walengwa,” amesema Silinde.
Leave a comment