MBUNGE wa Tandahimba (CUF), Katani Ahmed Katani, amevunja ukimya na kuutangazia ulikwengu kuwa hawezi kujiuzulu wazifa wake wa ubunge. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akizungumza bungeni mjini Dodoma jioni hii, Katani alisema, hajajiuzulu nafasi yake na wala hawezi kujiuzulu.
“Mheshimiwa Spika, napenda kuufahamisha umma kuwa mimi Katani Ahmed Katani, sijajiuzulu nafasi yangi ya ubunge. Sifikirii kujiuzulu na kwa hakika, siwezi kujiuzulu,” ameeleza Katani huku akishangiliwa na wabunge wenzake.
Mbunge huyo machachari katika eneo la kusini alieleza masikitiko yake jinsi vyombo vya habari, hasa Jamii Forum na mitandao mingine ya kijamii, iliyohaha mchana kutwa kupotosha umma.
Katani alitoa kauli hiyo, kufuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa mbunge wa CUF katika jimbo la Temeke, Abdallah Mtolea.
Alisema, “nimesikitishwa sana na hatua ya vyombo hivyo vya habari, kushupalia kuwa nimejiuzulu. Mimi nipo na nasikitika kwa nini hawajaniuliza,” ameeleza.
Alisema, “naviomba vyombo hivyo ili kulinda heshima yenu na kuitendea haki taaluma yenu, mniombe radhi kwa jinsi mlivyonichafua na mlivyoleta taharuki kwa wapigakura wangu.”
Katani alitoa kauli hiyo wakati akichangia muswada wa sheria ndogo ya fedha uliyowasilishwa bungeni mapema leo asubuhi na waziri wa fedha na uchumi, Dk. Philip Mpango.
Leave a comment