NI lazima Freeman Mbowe, Tundu Lissu na Zitto Kabwe watengeneze ‘kemistri’ kali ili kumkabili Rais John Magufuli, iwapo atateuliwa na chama chake (CCM) kuwaia urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2020. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 16 Oktoba 2019 na Ado Shaibu, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa ACT-Wazalendo alipoulizwa na mwandishi wa mtandao huu, kuhusu madai ya Zitto kutaka kumpora Lissu ili ajiunge na chama chake.
Mwandishi alimweleza Ado wasiwasi unaojengwa na baadhi ya makada wa Chadema, kuhusu ukaribu unaotengenezwa na Zitto ambaye ni Kiongozi Mkuu wa ACT-Wazalendo na Lissu, Mwanasheria Mkuu wa Chadema.
Hivi karibuni, Zitto amekuwa akimtembelea Lissu nchini Ubelgiji, na kufanya naye mazungumzo huku mshauri wa ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad akipongeza ukaribu wa wanasiasa hao wawili.
Mwandishi: Ukaribu wa Zitto na Lissu unaonekana kukua kwa kasi na hata, maofisa na wafuasi wa Chadema kujenga mashaka kwamba, Zitto anamwindi mwanasias huyo. Hili likoje?
Ado: Mashaka ya nini? Kumkabili Rais Magufuli kwenye uchaguzi mkuu ujao, kunahitaji nguvu kubwa. Ni lazima Mbowe, Lissu na Zitto watengeneze kemistri ‘muungano’ kali ili kumng’oa. Dhamira ya Zitto ipo hapo.
Ado amesema, ukaribu wa Zitto, Mbunge wa Kigoma Mjini na Lissu ni wa kisiasa hasa katika kipindi hiki siasa za Tanzania zilivyo ngumu. Amemtaja Lissu kuwa ni alama ya mapambano ya demokrasia nchini.
“Unajua Lissu ameweka rehani roho yake, anapigania maisha yetu dhidi ya utawala huu. Lazima wenye malengo yanayofanana waungane naye kwenye safari hiyo nzito. Zitto yupo kwenye malengo hayohayo ya Lissu na wapenda demokrasia,” amesema.
Lissu ambaye alikuwa mbunge wa Singida Mashariki, yupo nje ya nchi akipatiwa matibabu baada ya kushambuliwa kwa risasi ‘Area D’, Dodoma tarehe 7 Septemba 2017.
“Sio sahihi kuwaza Lissu atoke Chadema, lakini yeye ni mwanasiasa ambaye anaweza kuwa na matakwa yake mwenyewe. Kwa maoni yangu Lissu abaki Chadema na aungwe mkono,” amesema Ado.
Leave a comment