MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe anaongoza orodha ya wabunge wa chama hicho kushindwa kutetea ubunge wao katika majimbo mbalimbali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Sakaam … (endelea).
Matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika jana Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020, yameanza kutangazwa huku Mbowe aliyekuwa anatetea Jimbo la Hai Mkoa wa Kilimanjaro, Shaashisha Mafuwe wa CCM alishinda kwa kura 89,786 huku Mbowe akiambulia kura 27,684.
Wengine walioanguka ni; Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ (Mbeya Mjini),John Heche (Tarime Vijijini), Catherine Ruge (Serengeti), Esther Matiko (Tarime Mjini).
Mbowe ambaye alikuwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni alikuwa mbunge wa jimbo hilo kwa miaka kumi mfululizo.
Kwa upande wa Sugu, alishindwa baada ya kupata kura 37,591 dhidi ya mshindi wa jimbo la Mbeya Mjini kupitia CCM, Dk. Tulia Ackson aliyepata kira 75,225.
Sugu ambaye katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 alikuwa mbunge aliyepata kura nyingi kuliko mbunge yoyote, alikuwa anaongoza jimbo hilo kwa miaka 10 mfululizo.
Naye Heche ameangushwa na Mgombea wa CCM, Mwita Waitara aliyepata kura 35,758 huku mwanasiasa huyo akipata kura 18,757.
Heche aliongoza jimbo hilo jipya lililoanzishwa mwaka 2015 baada ya kugawanywa lile la Tarime.
Jimbo la Serengeti mkoa wa Mara, Catherine Ruge wa Chadema aliyekuwa mbunge wa viti maalum amepata kura 19,347 na Amsabi Mrimi wa CCM ameibuka mshindi kwa kupata kura 47,499.
Esther Matiko wa Chadema, ameshindwa kutetea jimbo hilo kwa awamu ua pili mfululizo baada Michael Kembaki wa CCM.
Endelea kufuatilia MwanaHalisi Oneline, MwanaHalisi TV na mitandao yetu ya kijamii kwa taarifa na habari mbalimbali za utangazaji wa matokeo yanayoendelea nchi nzima.
Leave a comment