MWENYEKITI wa Chadema, Freeman Mbowe na viongozi wenzake sita akiwemo Halima Mdee, Mbunge wa Kawe aliyeunganishwa katika kesi hiyo leo, wamekamilisha masharti ya dhamana hivyo wakati wowote wanaweza kuachiwa huru. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imejiridhisha na nyaraka walizoziwasilisha wadhamini kwa ajili ya dhamana ya washtakiwa hao na imewakubalia kuwadhamini huku ikiwapa maelekezo kuhakikisha kuwa wanapatikana mahakamani kila wanapohitajika.
Masharti ya dhamana yao ni kusaini bondi ya Sh 20 milioni kuwa na wadhamini wawili wenye barua kutoka ofisi za Serikali za mitaa au vijiji na kuripoti kituo kikuu cha Polisi kila Alhamisi.
Mbali ya Mbowe wengine ni Katibu Mkuu Dk Vicent Mashinji, manaibu katibu wakuu John Mnyika (Bara), Salum Mwalimu (Zanzibar), Mbunge wa Iringa Mjini Mchungaji Peter Msigwa na Mweka Hazina wa Baraza la Wanawake wa chama hicho, Ester Matiko na Mwenyekiti wake, Halima Mdee ambaye ni Mbunge wa Kawe, wanaokabiliwa na kesi ya jinai, wakidaiwa pamoja na mambo mengine ikiwamo kufanya mikusanyiko na maandamano yasiyo halali.
Kabla ya Mdee kupata dhamana pamoja na wenzake mawakili wa Serikali wapinga mahakama kumpa dhamana Mdee kwa sababu kabla hajafikishwa mahakamani alipewa dhamana Polisi lakini hakukidhi masharti kwa kushindwa kuripoti polisi wasema wanahofu akipewa dhamana ya mahakama hataweza kutimiza wajibu wake.
Hakimu Mkazi Wilbard Mashauri hakukubaliana na madai ya mawakili wa Serikali kwani Mahakama haiwezi kumnyima mshtakiwa dhamana kwa sababu aliruka dhamana ya polisi kwa kuwa hizo ni taasisi mbili tofauti na haziwezi kuingiliana.
Kesi hiyo itatajwa tena Aprili 16, 2018. Watuhumiwa hao walikuwa mahabusu tangu walipopandishwa kizimbani na kusomewa mashtaka hayo Machi 27 mwaka huu, 2018.
Leave a comment