FREEMAN Mbowe, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)-Taifa amesema kuwa, msiba wa Dk. Reginald Abraham Mengi ni msiba kwa taifa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Dk. Mengi ambaye ni mwenyekiti wa kampuni zilizo chini ya IPP Group amefariki usiku wa kuamkia leo tarehe 2 Mei 2019 akiwa Dubai, Falme za Kiarabu.
“Msiba huu ni hasara kwa taifa kutokana na umuhimu wa Dk. Mengi kwa Watanzania. Dk. Mengi ni miongoni mwa watu waliokuwa rafiki kwa vyama vyote vya siasa,” amesema Mbowe.
Kiongozi huyo wa Chadema ametoa kauli hiyo alipokuwa nyumbani kwa marehemu Mzee Mengi, Kinondoni jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kutoa salamu za pole.
Amesema kuwa, Dk. Mengi pamoja na kwamba ni mjomba wake pia rafiki wa vyama vyote vya siasa pia lakini ni rafiki wa masikini, watu wenye ulemavu na kila aina ya makundi ya watu.
Pia wamdishi wa habari kutoka mikoa mbalimbali waliopo jijini Dodoma kuhudhuria Maadhimisho ya Siku ya Vyombo vya Habari Dunia, wamesimama kwa dakika moja kutoa ishara ya heshima na kumkumbuka Dk. Mengi.
Nevile Meena, Katibu Mkuu wa Jukwaa la Wahariri (TEF) akiwa kwenye maadhimisho hayo amesema, kifo cha Dk. Mengi ni pigo kwa tasnia ya habari.
Leave a comment