UPANDE wa utetezi katika kesi ya uhujumu uchumi yenye mashtaka ya kula njama za kufanya ugaidi inayomkabili Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania cha Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu umesema, inatarajia kutumia mashahidi kadhaa wakiwemo, Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro na aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Peter Kibatala anayeongoza jopo la mawakili wa utetezi, ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam leo Jumatatu, tarehe 23 Agosti 2021, mara baada ya upande wa mashtaka kumaliza kuwasomea maelezo ya awali, Mbowe na wenzake watatu.
Mbali na Mbowe wengine; ni Halfan Bwire Hassan, Adam Hassan Kasekwa na Mohamed Abdallah Ling’wenya ambao wameieleza mahakama kwamba, maelezo waliyoyatoa polisi walilazimishwa.
Wakili Kibatala ameeleza hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Thomas Simba wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili ya kusomwa hati ya mashtaka na ushahidi kwa hatua za awali (Commital Proceeding).
Ni baada ya mkurugenzi wa mashtaka nchini (DPP) kuwasilisha taarifa hizo katika Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.Kibata ameieleza mahakama hiyo kwamba, upande wa utetezi katika kesi hiyo, unapendekeza majina mawili ya mashahidi wake, ambalo ni jina la IGP Sirro na Ole Sabaya.
“…ingependeza mahakama ichukue majina mawili ya mashahidi, la kwanza ni Lengai Ole Sabaya na la pili, IGP Simon Sirro,” amesema Kibatala.
Hata hivyo, Kibatala amesema upande huo utaleta mashahidi wengine wakati kesi hiyo inaendelea kusikilizwa.
Baada ya kutoa maelezo hayo, Hakimu Simba amesema mahakama hiyo imekamilisha usikilizwaji wa awali hivyo anaihamisha katika Mahakama Kuu, yenye mamlaka ya kuisikiliza kesi hiyo.
Kwa mujibu wa upande wa mashtaka, unatarajia kutumia mashahidi 24 na vielelezo vya maandishi 19.
Sabaya aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Hai Mkoa wa Kilimanjaro, alisimamishwa kazi na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizokuwa zinamkabili ikiwemo matumizi mabaya ya madaraka.
Na tayari amekwisha kupandishwa Mahakama ya Arusha akiwa na kesi mbili tofauti zikiwa na mashtaka uhujumu uchumi, kuendesha genge la uhalifu, matumizi mabaya ya madaraka, unyang’anyi wa kutumia silaha.
Asante sana kwa kutuhabarisha.
Nawatakia maandalizi mema sana ya habari zijazo.
Rafiki yenu,
Aliko Musa
Mbobezi Kwenye Majengo.