MAKAMU Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)- Tanzania Bara, Tundu Lissu amesema, anashauriana na viongozi wa chama hicho, namna ya kurudi nchini humo ili aendelee na majukumu yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya Freeman Mbowe, kushikiliwa na Jeshi la Polisi, kwa tuhuma za ugaidi na kupanga njama za kuua viongozi wa serikali.
Mbowe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema Taifa, anashikiliwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, baada ya kukamatwa akiwa katika Hoteli ya Kingdom, jijini Mwanza, usiku wa kuamkia tarehe 21 Julai 2021.
Akizungumza na wanahabari kwa njia ya mtandao ‘Zoom’ leo Ijumaa tarehe 23 Julai 2021, Lissu amesema, muda si mrefu atarejea Tanzania, akitokea nchini Ubelgiji, alikokwenda baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2020.
“Nimeshasema kwamba, nitarudi nyumbani muda si mrefu na kwa hali ilivyo itabidi tufanye mawasiliano na mashauriano na viongozi, ni muda gani mzuri kurudi nyumbani,” amesema Lissu.
Aidha, Lissu amesema, ataendelea kuiongoza Chadema akiwa ughaibuni, kupitia njia ya mtandao, kama alivyoongoza kikao cha dharura cha Kamati Kuu ya chama hicho, kilichofanyika kwa njia ya mtandao, jana tarehe 22 Julai 2021.
“Kwa sababu hiyo, inawezekana yale ambayo yalikuwa hayawezekani zamani wakati hakukuwa na njia za kisasa za mawasiliano. Sasa yanawezakana, kwa hiyo hata nikiwa Ubelgiji shughuli za chama na vikao vya chama vitaendelea tu,” amesema Lissu.
Lissu aliyekuwa Mgombea Urais wa Chadema, katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana, Novemba 2020, alirudi nchini Ubelgiji alikokwenda kwa ajili ya kupatiwa matibabu, Januari 2018.
Lissu alipelekwa Ubelgiji kwa matibabu baada ya kunusurika kifo, kufuatia kupigwa risasi na watu wasiojulikana, tarehe 7 Septemba 2017, jijini Dodoma. Julai 2020 alirudi Tanzania kushiriki uchaguzi mkuu.
Leave a comment