FREEMAN Mbowe, mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kupumzika kutokana na hali ya afya yake kutoimarika. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mbowe na wenzake wanane wanashtakiwa kwenye mahakama hiyo kwa mashitaka 13 yakiwemo kufanya kusanyiko kinyume cha sheria, kutoa maneno ya uchechezi na kusababishia kifo Akwiline Akwilina, mwanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Chuo cha Usafirishaji cha taifa (NIT).
Washtakiwa wengine katika kesi hiyo, ni Dk. Vecent Mashinji, katibu mkuu wa chama hicho; John Mnyika, naibu katibu mkuu (Bara); Salum Mwalim, naibu katibu mkuu Zanzibar na Halima James Mdee, mbunge wa Kawe na mwenyeti wa Baraza la Wanawake la chama hicho (BAWACHA).
Wengine waliomo kwenye kesi hiyo, Na. 112 ya mwaka 2018, ni Ester Matiko, mbunge wa Tarime Mjini;
Peter Msigwa, mbunge wa Iringa Mjini, John Heche, mbunge wa Tarime Vijijini na Ester Bulaya, mbunge wa Bunda Mjini.
Akiwasilisha maombi ya kutoendelea kwa kesi hiyo, wakili wa Mbowe, Jeremiah Mtobesya, alimueleza Hakimu Mkazi Mkuu wa mahakama hiyo, Thomas Simba, kwamba Mbowe alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa Homa ya Dengue, Malaria na shinikizo la damu na kwamba ameruhusiwa kutoka hospitali siku ya Ijumaa tarehe 22 Novemba 2019.
Amesema, pamoja na kutoka hospitali, hali ya mwanasiasa huyo wa upinzani, bado haijatengemaa. Akaomba kuarishwa kwa shauri hilo ilia pate muda wa kupumzika.
Hata hivyo, upande wa mashitaka unaoongozwa na Wakili Mkuu wa Serikali, Faraja Nchimbi, umepinga maombi hayo.
Nchimbi amedai, afya ya Mbowe imekaa sawa na kwa kuwa shauri hilo limekuwa likikwama kwa sababu kama hizo, ameiomba mahakama kuendelea kusikiliza shauri hilo.
Baada ya kusikiliza pande zote mbili, Hakimu Simba amedai, suala la afya ni muhimu kwa kila binadamu na hivyo anaaihirisha sahuri hilo, hadi tarehe 28 Novemba 2019.
Leave a comment