LEO Jumatatu tarehe 14 Februari 2022 ni siku ya wapendao ‘Valentine Day’ na ndani ya chumba cha Mahakama Kuu, Divisheni ya Rushwa na Uhujumu Uchumi jijini Dar es Salaam, rangi nyekundi imetawala. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Baadhi ya wanachama wa Chadema, wamejitokeza wakiwa wamevalia tisheti zenye ujumbe ‘Happy Valentine Day Freeman Mbowe.’
Mbowe na wenzake watatu wanakabiliwa na kesi ya ugaidi mahakamani hapo ambapo washtakiwa wote wanne, nao wameingia ndani ya chumba hicho wakiwa wamevalia tisheti nyekundi.
Kama ilivyokawaida, Mbowe anapoingia baadhi ya wahudhuriaji hususan wa Chadema husikama kuonesha heshima kwa kiongozi wao na amewasalimia kisha akamalizia kwa kusema “Kheri ya Valentine.” Kisha wakaitikia na kwako pia.
Sauti ya mwanamke ikasikika ikisema ‘umependeza saaaana.”
Leo Jumatatu, shahidi wa 13 wa Jamhuri ambaye ni Askari Polisi, Tumain Swila anatarajia kuendelea kutoa ushahidi wake baada ya kuugua ghafla akiwa kizimbani tarehe 9 Februari 2022.
Mara baada ya kuugua, Jaji Joachim Tiganga aliahirisha kesi hiyo hadi tarehe 10 Februari 2022 ambapo siku hiyo mawakili wa serikali waliieleza Mahakama ya Kuu, Divisheni ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam kwamba daktari amemshauri kupumzika siku tatu katika Hospitali ya TMJ, Dar es Salaam.
Mbali na Mbowe, washtakiwa wengine katika kesi hiyo yenye mashtaka sita ya ugaidi ni, waliokuwa makomando wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Halfan Bwire Hassan, Adam Kasekwa na Mohammed Abdillah Ling’wenya.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI TV, MwanaHaLISI Online na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali
Leave a comment