Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Mbowe atoa msimamo kurudi bungeni, kukatwa fedha
Habari za Siasa

Mbowe atoa msimamo kurudi bungeni, kukatwa fedha

Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema Taifa
Spread the love

FREEMAN Mbowe, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni nchini Tanzania, amesema linapokuja suala la usalama wa maisha, pesa haina thamani. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).

Akizungumza na Shirika la Utangazaji la Uingereza (BBC), Mbowe amesema wabunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), hawajali kukatwa fedha kutokana na kutohudhuria vikao vya Bunge vinavyoendelea jijini Dodoma.

“Hatutajali kama hawatatulipa pesa zetu kwa kutohudhuria bungeni, sababu ni suala linalohusu maisha yetu na sio pesa,”  amesema Mbowe.

Mbowe amesema hatua ya Chadema kuzuia wabunge wake kuhudhuria vikao vya bunge, ili kukaa karantini kwa siku 14 kuanzia tarehe 1 Mei 2020 ili kuangalia kama wana maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19) au la ilitokana na vifo vya wabunge watatu vilivyotokea ndani ya wiki mbili.

Wabunge hao waliofariki ni Getrude Mongella, Viti Maalum (CCM), Richard Ndassa wa Sumve (CCM) pamoja na Balozi Augustine Mahiga, aliyekuwa waziri wa katiba na sheria.

Kiongozi huyo ametoa kauli hiyo ikiwa siku chache kupita tangu Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai kuwataka wabunge wa Chadema waliojiweka karantini kurejea bungeni haraka na endapo watakaidi wanafikiria kuwakata mishahara yao kwa kuwahesabu kama ni watoro.

Katika mahojiano hayo na BBC, Mbowe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema, amesema Serikali ya Tanzania haitumia njia za kisayansi katika kupambana na janga hilo, badala yake inauona ugonjwa wa COVID-19, kama ni ugonjwa mdogo.

Amesema namna Serikali inavyoshughulikia COVID-19, inaweza gharimu maisha ya watu pamoja na sekta ya uchumi.

“Mgogoro wetu na Serikali ni namna inavyoshughulikia janga hili. Serikali au Rais John Magufuli hataki kukubali kama Corona ni tatizo, bali inauona kama ugonjwa mdogo. Anaona maombi yanaweza saidia kutatua tatizo,” amesema Mbowe

“Lakini tulimwambia suala hili linahitaji suluhisho la kisayansi, lakini jinsi anavyoshughulikia janga hili, inaweza kugharimu uchumi na watu wetu.”

Kuhusu suala la vipimo vya COVID-19 kuwa na dosari, Mbowe amesema Serikali ilipaswa kuvichunguza kabla ya kuruhusu vitumike.

“Kama vipimo vina dosari, ni suala ambalo serikali ilipaswa kujua muda mrefu kabla ya kutumiwa,” amesema Mbowe.

Suala la vipimo hivyo vilikosolewa na Rais John Magufuli wakati wa hafla ya kumwapisha Dk Mwigulu Nchemba kuwa waziri wa katiba na sheria iliyofanyika tarehe 3 Mei 2020 nyumbani kwake, Chato mkoani Geita.

Miongoni mwa kasoro ambazo Rais Magufuli alizieleza juu ya majibu ya vipimo vya corona ni sampuli za mapapai, mbuzi kuonyesha kuwa na corona hali aliyotaka uchunguzi ufanyike ili kubaini ukweli wake.

 

Hata hivyo, Mbowe amekosoa kitendo cha nchi kuwa na maabara moja inayopima ugonjwa huo, kwa kuwa ina idadi kubwa ya wananchi wanaohitaji huduma hiyo.

“Maabara ya taifa ina udhaifu katika kufanya vipimo, tuna maabara moja iliyoko jijini Dar es Salaam, inayohudumia watu zaidi ya milioni 50,” amesema Mbowe.

Kiongozi huyo wa chama kikuu cha upinzani nchini, ameitaka Serikali kutoka hadharani na kueleza hali halisi kuhusu athari za janga hilo hapa nchini.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

Habari za Siasa

CCM yamkana mwenyekiti UVCCM aliyetaka wapinzani wapotezwe

Spread the love  CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimejitenga na kauli ya mwenyekiti...

Habari za SiasaTangulizi

Rais Samia kutunukiwa udaktari wa heshima Uturuki

Spread the loveBaraza la Chuo Kikuu cha Ankara, ambacho ni cha pili...

error: Content is protected !!