FREEMAN Mbowe, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amesema atamkumbuka aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano wa Tanzania, Hayati Dk. John Magufuli kwa mambo mawili. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na Watanzania kupitia mitandao ya kijamii leo tarehe 11 Aprili 2021, ametaja mambo hayo kuwa ni kufanya uamuzi mgumu na pili; kuchapa kazi kwa bidii.
“Hayati Magufuli, rais wetu aliyetutoka atakumbukwa kwa mengi, mabaya na mazuri katika muktadha wa utawala na uongozi wa nchi.
“Nayajua mambo mawili ambayo nadiriki pasipo shaka kusema ni mazuri, tunayoweza kumkumbuka nayo ambayo aliyaishi kwa ukamilifu wake na aliyatenda bila kujali na kuogopa athari zake,” amesema Mbowe.
Mbowe ameendelea “sifa za kipee za Rais Magufuli ni moja, uthubutu wa kufanya maamuzi magumu. Alikuwa na uwezo wa kufanya maamuzi ambayo busara za kawaida za binadamu usingeweza kufanya. Alikuwa na kipaji hicho.
Mbowe amesema, sifa ya pili ni kuhimiza Watanzania kufanya kazi kwa bidii, huku akisema kwamba mwanasiasa huyo aliishi falsafa ya Chadema inayosema ‘asiyefanya kazi na asile.
“La pili aliamini na kusisitiza katika uchapakazi kufanya kazi kwa bidii, alikuwa si mtu mvivu, alijituma, alifanya kazi usiku na mchana. Alisisitiza watu kufanya kazi na aliishi fisolosofia ya Chadema, asiefanya kazi na asile. Jambo hilo tunalikubali,” amesema Mbowe.
Hayati Magufuli aliongoza Tanzania kwa miaka mitano na miezi mitano mfululizo (Novemba 2015 hadi Machi 2021), kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Kiongozi huyo alifariki dunia tarehe 17 Machi 2021, kakita Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam, alikokuwa anapatiwa matibabu ya ugonjwa wa mfumo wa umeme wa moyo. Alizikwa nyumbani kwao Chato mkoani Geita, tarehe 26 Machi mwaka huu.
Na mabaya aliyosema mbona mnayaficha? Kwanini msituwekee video yake? Acheni kufanya kazi kama gazeti la Uhuru