MWENYEKITI wa Chama cha Chadema, Freeman Mbowe, amewasili nyumbani kwao wilayani Hai, Kilimanjaro na kupokelewa na mamia ya watu ikiwemo viongozi na wanachama wa chama hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro…(endelea).
Mbowe amewasili nyumbani kwao leo Jumamosi, tarehe 19 Machi 2022, majira ya saa 3 asubuhi kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), akitokea Dar es Salaam.
Wakati anawasili uwanjani hapo, alipokewa na baadhi ya viongozi wa Chadema wa Taifa, kanda na mkoa huo, ambapo wanachama na wananchi wa kawaida walizuiwa kuingia ndani kutokana na sababu za kiusalama.
Akiwa njiani kueleka nyumbani kwao Hai, katika njia panda ya KIA, Mbowe alisimamishwa na kundi la watu lililojipanga pembezoni mwa barabara hiyo kwa ajili ya kumsalimia.
Mbowe aliwasalimu “hamjambo ndugu zangu,”na wenyewe walimjibu wakisema “hatujambo” kisha akaendelea kusema “nimewa-miss sana, ahsanteni sana kwa kunipokea tuko pamoja. Tuendelee.”
Katibu wa Chadema wilayani Mwanga, Lembruse Mchome, amesema kuna wananchi wametoa ng’ombe sita , ambao watachinjwa kwa ajili ya kumpokea Mbowe.
“Kama mnavyojua tuko kwenye maandalizi mazito ya kumpokea mwenyekiti, maandalizi yanaendelea hapa nyumbani machame, tunatarajia kuchinja ng’ombe wasiopungua sita na ambao wameletwa na wazee na wanachama kama zawadi ya kumpokea,” amesema Mchome.
Kesho Jumapili, tarehe 20 Machi 2022, Mbowe anatarajia kufanya ibada ya shukrani, ya kuachwa huru baada ya kusota rumande kwa zaidi ya siku 200, kufuatia hatua ya Mahakama Kuu,Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam, kumfutia mashtaka ya ugaidi yaliyokuwa yanamkabili.
Hatua ya mahakama hiyo kumfutia mashtaka Mbowe na walinzi wake watatu, Halfan Bwire Hassan, Adam Kasekwa na Mohammed Abdillah Ling’wenya, ilitokana na Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), Sylvester Mwakitalu, kuwasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea nayo.
Nibure tu kukosa pia kazi