FREEMAN Mbowe, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo ametangazwa tena kuhudumu nafasi hiyo kwa awamu nyingine. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Akitangaza matokeo hayo, Msimamizi wa Uchaguzi, Sylivester Masinde, alisema Mbowe ameshinda kwa kura 886 sawa na asilimia 93.5 dhidi ya Cecil Mwambe aliyepata kura 59 sawa na asilimia 6.2.
Kwa upande wa Makamu Mwenyekiti wa chama Zanzibar, Mgombea alikuwa ni mmoja ambaye ni Said Mohamed na ameshinda nafasi hiyo kwa kura za ndio 839 sawa na asilimia 88.7, kura za hapana 95 sawa na asilimia 10, kura zilizoharibika ni 12 sawa na asilimia 1.3.
Makamu Mwenyekiti Bara wagombea walikuwa wawili ambapo mgombea Sophia Mwakagenda wakati akijinadi alitangaza kumuachia kiti hicho Tundu Lissu agombee lakini kwa kuwa karatasi za kura zilishawekwa jina lake na kulikuwa na watu wanaomtegemea kumpa kura hivyo kura zikapigwa akijumuisha na yeye.
Baada ya hatua hiyo, Mwakagenda alipata kura 11 sawa na asilimia 1.2, Tundu Lissu alipata kura 930 sawa na asilimia 98.8 na kura zilizoharibika zilikuwa tisa sawa na 0.9 hivyo Tundu Lissu amekuwa Makamu Mwenyekiti wa chama hicho upande wa Bara.
Katika uchaguzi huo kura zilianza kupigwa jana tarehe 18 Desemba 2019 saa saba usiku licha baada ya muda mfupi baada ya zoezi hilo kuanza umeme ulizimika ndani ya ukumbi wa mikutano na kupelekea zoezi hilo kusimama kwa muda. na haikujulikana nini chanzo.
Zoezi la uchaguzi lilikamilika alfajiri ya saa 11 na dakika 25 leo tarehe 19 Desemba 2019 na washindi walipata nafasi ya kutoa hutuba ya shukrani kwa wajumbe, isipokuwa Lissu ambaye yupo nje ya nchi ambaye awali alijinadi kupitia mtandao wa Whatsapp (video call).
Leave a comment