MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, amesema hana ugomvi na shahidi wa Jamhuri, Innocent Mdowo (37), kwani ni “ndugu yangu sina ugomvi naye. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mbowe ambaye ni mshtakiwa wa nne kwenye kesi ya ugaidi inayoendelea Mahakama Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, jijini Dar es Salaam, ameeleza hayo wakati akiwasalimia watu mbalimbali waliofika mahakamani kusikiliza kesi hiyo.
Mwanasiasa huyo imekuwa kawaida yake kila anapoingia ndani ya chumba cha mahakama, huwasalimia watu wote wakiwemo mawakili wa pande zote yaani wa wanaomtetea na wa serikali.
Leo Alhamisi, tarehe 20 Januari 2022, Mbowe na wezake watatu kwenye kesi hiyo, Halfan Bwire Hassan, Adam Kasekwa na Mohammed Abdillah Ling’wenya, ambao waliwahi kuwa makomandoo wa Jeshi la Ulinzi na Wananchi wa Tanzania (JWTZ), mara baada ya kuingia alianza kusalimia kundi moja baada ya jingine.
Mbowe alimsalimia kiongozi wa Jopo la Mawakili wa Jamhuri, Robert Kidando na Kiongozi wa Jopo Mawakili wa Utetezi, Peter Kibatala na kumuacha shahidi wa Jamuri, Innocent Ndowo, aliyekuwepo kortini.
Ndipo wafuasi wa Chadema walivyomkumbusha wakimwambia “Mwenyekiti umemsahau shahidi.” Huku wakicheka.
Baada ya wafuasi hao kutoa kauli hiyo, Mbowe alidai Inspekta Ndowo ni ndugu yake, hivyo hana ugomvi naye.
“Kidando nakuona mkuu wasalimie wenzako, Kibatala nawe nakuona. Shahidi ndugu yangu sina ugomvi naye,” amedai Mbowe.
Shahidi huyo aliyekuwepo ameketi katika benchi la mahakama hiyo, hakujibu.
Wakati anatoa ushahidi wake mahakamani hapo, mbele ya Jaji Joachim Tiganga, Ndowo ambaye ni askari polisi aliyebobea eneo la uchunguzi wa kisayansi alisoma meseji zilizopatikana katika mtandao wa Telegram, zinazodaiwa kuwa ni mawasiliano kati ya Mbowe na Denis Urio, anayedaiwa kumtumia kutafuta makomandoo wa JWTZ.
Katika meseji hizo zilizosomwa na Inspekta Ndowo, zinaonesha namna mtu anayedaiwa kuwa ni Mbowe, alivyowasiliana na Urio kwa ajili ya kumtafutia vijana wa kazi.
Pia, meseji hizo zilionesha namna mtu anayedaiwa kuwa Mbowe na Urio, waliwasiliana juu ya namna ya kutumiana fedha za kuwasafirisha vijana hao kutoka mikoani kuja Dar es Salaam na kwenda wilayani Hai, Mkoa wa Kilimanjaro.
Shahidi huyo anaendelea kutoa ushahidi wake.
Leave a comment