LENGAI Ole Sabaya, Mkuu wa Wilaya ya Hai, Kilimanjaro anatajwa kama mtu mnyanyasaji kwa wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Anaripoti Mwandishi Wetu, Hai … (endelea).
Freeman Mbowe, Mbunge wa Hai na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, anamtuhumu Sabaya na polisi wilayani humo kuendesha vitisho na kuwatia hofu wafuasi wake.
Kiongozi huyo wa Chadema, licha ya kukamatwa na kuachwa kwa dhana siku mbili zilizopita amesema, Hai kuna vitisho dhidi ya wale wasio na mahaba na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara jimboni kwake katika viwanja vya Snow View, Mbowe amedai, Sabaya amekuwa akiwabambikia kesi wananchi wasiokuwa na hatia.
Kutokana na kile alichoita ‘tabia ya Sabaya,’ amemtaka DC huyo kuacha kunyanyasa wafuasi wa upinzani.
Amesema, miongoni mwa wanaokumbwa na dhahama ya Sabaya ni kundi la vijana wa bodaboda wanaomuunga mkono yeye (Mbowe).
“DC anabambikizia watu kesi zisizokuwa na msingi,” amesema Mbowe.
Amesema, Sabaya amekuwa akikamata vijana wa Chadema kwa madai ya kuharibu miundombinu ya reli bila ushahidi wowote.
“Anatuhumu watu kuharibu miundombinu ya reli jambo ambacho si kweli, vijana wa bodaboda Hai hawaishi kwa amani, kisa wanamuunga mkono Mbowe,”am amesema.
Pia Mbowe amemtuhumu Sabaya kwenda kwenye vituo vya bodaboda na kuwazuia kumpokea.
” Eti wasimpokee mbunge wao, mambo gani ya kihuni haya?” amesema
Mbunge huyo ameonya kuendelea kwa tabia hiyo Hai, na kwamba kinachomneemesha Sabaya kutoka kwa wananchi ni heshma ya ukuu wa wilaya.
Leave a comment