HAKIMU Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam, Wilbard Richard Mashauri, ni miongoni mwa maofisa 15 wa mahakama waliotangazwa na Rais John Pombe Magufuli, kuwa majaji wa Mahakama Kuu. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Hakimu Mkuu Mkazi Mashauri, ndiye anayesikiliza kesi ya jinai inayowakabili viongozi wandamizi wa Chama cha Maendeleo na Demokrasia (CHADEMA), wakiongozwa na mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe.
Wengine kwenye kesi hiyo, ni Dk. Vicenti Mashinji, katibu mkuu wa chama hicho; Halima James Mdee, mbunge wa Kawe na mwenyekiti wa baraza la wanawake la Chadema (Bawacha); John Mnyika, mbunge wa Kibamba na naibu katibu mkuu (BARA) na John Heche, mbunge wa Tarime Vijijini.
Wengine, ni Salum Mwalimu, naibu katibu mkuu wa chama hicho Zanzibar; Mchungaji Peter Msigwa, mbunge wa Iringa Mjini; Esther Matiko, mbunge wa Tarime Mjini na mweka hazina wa Bawacha taifa na Ester Bulaya, mbunge wa Bunda.
Viongozi hao wakuu wa Chadema wanashitakiwa katika mahakama hiyo kwa kosa la kufanya maandamano, siku moja kabla ya kufanyika uchaguzi mdogo wa ubunge katika jimbo la Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Alikuwa ni Hakimu Mashauri ambaye tarehe 23 Novemba mwaka jana, alimua kuwafutia dhamana Mbowe na Matiko kwa madai ya “kuidharau mahakama.”
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi, mbali na uteuzi huo wa majaji wa Mahakama Kuu, Rais Magufuli, ameteuwa majaji wawili wa mahakama ya rufaa; wakurugenzi 10 wa halmashauri za wilaya na wakuu wa wawili wa wilaya.
Aidha, rais amefuta uteuzi wa wakuu wa wilaya wawili – Glourious Luoga, aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Tarime mkoani Mara na Aaron Mbogho, aliyekuwa mkuu wa wilaya ya Mwanga, mkoani Kilimanjaro.
Taarifa kamili ya majaji walioteuliwa, wakurugenzi na wakuu wa wilaya walioteuliwa na wale “waliotumbuliwa,” soma hapa chini.
Leave a comment