KLABU za Mbao FC pamoja na Mbeya City zinashuka dimbani leo katika michezo ya marudiano ya mtoano (Play off) katika harakati za kuwania kusalia Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu ujao wa 2020/21. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Michezo ya mzunguko wa kwanza Mbao FC ilipoteza kwa mabao 2-0 dhidi ya Ihefu kutoka Mbeya, huku Mbeya City ikilazimshwa sare ya bao 1-1 na Geita Gold kutoka Shinyanga.
Katika michezo Mbao FC itakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa CCM Kirumba dhidi ya Ihefu huku ikiitaji ushindi wa mabao matatu ili iweze kusalia kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu ujao.
Kwa upande wa Mbeya City nao watakuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Sokoine kujiuliza mbele ya Geita Gold kwa kuhitaji sare ya bila kufungana au kupata ushindi wowote ili iweze kusalia kwenye Ligi Kuu kwa msimu ujao.
Ligi Kuu Tanzania Bara tayari imeshamalizika wiki iliyopita huku klabu za Alliance, Ndanda FC, Lipuli FC na Singida United zikishuka daraja huku klabu za Gwambina na Dodoma United zikipanda Ligi Kuu kwa msimu ujao.
Leave a comment