CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimesema hatua ya Rais Samia Suluhu Hassan kufanya mazungumzo na wapinzani haiwezi kumaliza changamoto zinazoikabili nchi kwenye demokrasia, kwani huenda akakwamishwa na baadhi ya watu wa chama chake cha CCM. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumatatu, tarehe 7 Machi 2022 na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, akihojiwa kwa njia ya mtandao na kituo cha runinga cha TV47 cha nchini Kenya.
Hapa Tanzania safari bado mbichi, hatuwezi kujenga hitimisho kwamba tunaona mwanzo mpya. Tunachokiona ni dalili tu za utashi wa kisiasa kwa upande wa kiti cha urais,” amesema Ado.
Ado amesema “Rais Samia atakuwa na wakati muhimu kwake kihistoria kuijenga demokrasia na kuijenga Tanzania, ambayo imeharibika sana katika miaka sita iliyopita. Lakini ili aweze kuruka kihunzi hicho vizuri, atalazimika kushinda mambo mengi, kushinda wahafidhina ndani ya CCM ambao hawatataka mabadiliko ya msingi yafanyike.”
Amesema kuwa, ili changamoto za kiuongozi zinazoikabili nchi ziishe, lazima utendaji wa mihili ya Serikali na taasisi za umma, uimarishwe.
“Jambo la msingi ni kwamba, haya ni masuala yanayopaswa kufanywa katika kipindi cha mpito, lengo mama linapaswa kuwa kuimarisha tasisi za umma. Ni lazima tutoke kwenye siasa za watu twende kwenye siasa za uendeshaji wa nchi kitaasisi,” amesema Ado.
Katibu mkuu huyo wa ACT-Wazalendo amesema “tukiwa na Bunge tuwe na Bunge madhubuti lenye madaraka yake kwa mujibu wa katiba na liweze kujisimamia, vivyo hivyo kwa Serikali, mahakama na tume ya uchaguzi. Hili ni jambo muhimu sana.”
Aidha, Ado amesema Rais Samia amejitofautisha na mtangulizi wake, Hayati John Magufuli, kwa kufanya maridhiano na wapinzani wake.
“Ambacho kipo bayana ni kwamba, Rais Samia amejitofautisha sana na mtangulizi wake, Rais Magufuli, hotuba ya mwanzo baada ya kuapishwa rasmi ilizungumzia juu ya kufungua ukursa mpya na vyama vya upinzani na kama mnavyofuatilia kwa karibu mmeona amekuwa akikutana na wapinzani,” amesema Ado.
Ikiwa zimesalia siku takribani 12 kuhitimisha mwaka mmoja kuwa madarakani, Rais Samia amefanya mazungumzo na wanasiasa wa upinzani pamoja na viongozi wa dini walio mstari wa mbele katika kuikosoa Serikali inapokwenda mrama.
Hivi karibuni, Rais Samia alifanya mazungumzo na Makamu Mwenyekiti wa Chadema Bara, Tundu Lissu, nchini Ubelgiji, kisha wiki mbili baadae alizungumza na mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe, muda mfupi baada ya kuachwa huru kutoka mahabusu ya Gereza la Ukonga, jijini Dar es Salaam.
Leave a comment