MSHAMBULIAJI wa klabu ya Yanga, Fiston Mayele amefunguka sababu zilizofanya kushindwa kupachika bao lolote katika michezo minne ya Ligi Kuu Tanzania Bara, huku akilalamika kuwa wachezaji wengi wanamkamia. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dodoma … (endelea).
Mchezaji huyo ameyasema hayo, mara baada ya kukamilika kwa dakika 90 za mchezo wa Ligi Kuu Bara kati ya Yanga dhidi ya Dodoma Jiji, uliopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri ambapo Yanga ilifanikiwa kuondoka na ushindi wa mabao 2-0.
Akitoa ufafanuzi kuhusu ukame wa mabao unaomuandama, Mayele alisema kuwa hilo ni jambo la kawaida kwenye mchezo wa mpira, ila kwa sasa wanaangalia matokeo ya timu kuliko yeye kufunga.
“Hilo ni jambo la kawaida kwenye mpira, mabao yatakuja tu ila kwa sasa tunaangalia malengo ya timu zaidi kuliko mimi kufunga.
“Tulicheza mechi tatu bila ushindi, sisi tunataka ubingwa hatuwezi kucheza michezo minne bila kushinda,” alisema Mayele.
Katika mchezo huo dhidi ya Dodoma Jiji, mabao ya Yanga yakiwekwa kamiani na Dickson Ambundo dakika ya 11 na bao la pili likifungwa na Zawadi Mauya dakika ya 34.
Licha ya kutofunga katika michezo minne mfululizo, mshambuliaji huyo bado ndio kinara katika orodha ya wafungaji kwenye Ligi Kuu kwa msimu huu, ambapo mpaka sasa amefanikiwa kupachika mabao 12, sawa na George Mpole wa Geita Gold.
Aidha Mayele aliendelea kusema kuwa, mabeki wengi.wa Ligi Kuu kwa sasa wanamkamia ili asifunge lakini anashukuru katika mazingira hayo yote timu yake ilifanikiwa kuondoka na alama.
“Mabeki wananikamia Fiston nisiteteme, lakini nashukuru tumeibuka na ushindi,” alisema mshambuliaji huyo
Kabla ya kukutwa na hali hii ya ukame wa mabao, Mayele alifanikiwa kufunga katika michezo sita mfululizo ya Ligi Kuu Bara
Leave a comment