PROFESA Ibrahim Juma, Jaji Mkuu wa Tanzania, ameahidi kuwachukulia hatua mawakili wanaopotosha maamuzi ya mahakama. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ametoa onyo hilo leo tarehe 21 Desemba 2020, katika hafla ya uapisho wa mawakili wapya 166, iliyofanyika kwenye viwanja vya Karimjee, jijini Dar es Salaam.
“Kazi ya wakili sio kupotosha maamuzi ya mahakama, kwa bahati nzuri kanuni za maadili zipo na zitatumika hata katika mitandao ya kijamii,” amesema.
Akizungumza katika hafla hiyo, Prof. Juma amesema kuna baadhi ya mawakili hukiuka maadili ya taaluma zao kwa kupotosha tafsiri za amuzi wa mahakama, kupitia mitandao ya kijamii hasa twitter.
“Kuna mawakili wachache ambao bado hawaziishi kanuni za maadili, nidhamu na tabia njema inayotarajiwa kwa mawakili.
“Kila siku katika mitandao ya kijamii hasa twitter, tumeona wakitumia lugha zisizofaa, wengine waziwazi na wengine kwa majina ya kubuni, wamejipambanua kwa kupotosha tafsiri za hukumu badala ya kuzifafanua,” amesema Prof. Juma.
Sambamba na hilo, Prof. Juma amesema, ofisi yake inapokea malalamiko mengi kutoka kwa wananchi kuhusu ukiukwaji wa maadili unaofanywa na baadhi ya mawakili wasio waaminifu.
Na kwamba, kuna baadhi ya mawakili hutumia vibaya taaluma zao kuchelewesha kesi kwa makusudi ili kuwapendelea wateja wao, kinyume na sheria.
“Hata hivyo, wako mawakili wana sifa za ujanja wa kuwasaidia wateja wao kukiuka maadili kwa makusudi na kuchelewesha kesi, sidhani kati ya mawakili wapya 166 wako mawakili wa aina hiyo,” amesema na kuongeza:
“Yapo pia malalamiko yanaonesha baadhi ya mawakili kupokea malipo, baadaye wakili huyo huona ni madogo, hayatoshi kadri kesi ilivyokuwa ikiendelea mahakamani, huanza kusumbua wateja wao na kukata mawasiliano kabisa,” amesema.
Amesema, wakati mwingine huzuia majalada na kuzuia wateja hao kutafuta mawakili wengine au kuendesha kesi wenyewe.
Kufuatia changamoto hiyo, Prof. Juma amewaasa mawakili wapya kuwa wabunifu kwa kuongeza ujuzi kuhusu taaluma yao, ili wakidhi soko la ajira.
“Kwa mujibu wa ripoti ya Jukwaa la Uchumi Duniani la Januari 2016, lilisema utaalamu na ujuzi mbalimbali ulioko duniani pamoja na ujuzi wa sheria tunaosoma, utatoweka hivi karibuni, kwa hiyo elimu mliyoipata inatakiwa kuendelezwa ili iweze kupambana na mazingira mapya ya ushindani wa karne ya 21,” amesema Prof. Juma.
Jaji huyo wa Tanzania amewataka mawakili wapya kujiandaa kukabiliana na changamoto ya ajira.
“Kuna jambo lingine ambalo sina budi kulizungumzia, suala la ajia katika karne ya 21, ingawa leo ni siku ya furaha, kwenu hapana shaka haifuti wasiwasi na hofu ya mawakili wengi na wanasheria kuhusu ajira za mawakili katika ushindani wa karne hii ya 21.
“Katika hotuba yangu ya kupokea mawakili tarehe 10 Julai mwaka huu, nilizungumzia changamoto ya ajira inayowakabili mawakili wapya, nilisema siku hizi ni jambo la kawaida wanasheria wanaokubaliwa kuwa mawakili hukosa kabisa ajira katika taasisi za umma ambazo zamani zilikuwa zinaajiri asilimia kubwa ya wahitimu wa sharia,” amesema.
Leave a comment