MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imeahirisha shauri namba 112 la mwaka 2018 la uchochezi linalowakabili viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo kutokana na kukosekana kwa mawakili vinara kwenye safu ya utetezi. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mawakili hao ni pamoja na Kiongozi wa Jopo, Profesa Abdallah Safari, Peter Kibatala na Hekima Mwasipu.
Kwenye kesi hiyo viongozi tisa akiwemo Freeman Mbowe , Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, DK. Vicent Mashinji, Katibu Mkuu, Jonh Mnyika, Naibu Katibu Mkuu Bara, Salum Mwalim, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar.
Wengine ni Halima Mdee, Mbunge wa Kawe, Mchungaji Peter Msigwa, Mbunge wa Iringa Mjini, John Heche, Mbunge wa Tarime Vijijini, Ester Matiko, Mbunge wa Tarime Mjini na Ester Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini.
Awali tarehe 8 Novemba 2019, Faraja Nchimbi, wakili wa Serikali Mkuu aliomba mahakama kuwa atamhoji Mbowe kupitia kielelezo namba tano (Min-Div) tepu yenye video iliyodaiwa kurekodi matukio yaliyotokea kwenye ufungaji wa kampeni za uchaguzi mdogo kwenye jimbo la Kinondoni tarehe 16 Februari, 2018.
Leo tarehe 13 Novemba 2019, shauri hili lilipangwa kuendelea kusikilizwa, Mbowe alitarajiwa kuendelea kutoa utetezi wake kwa kuhojiwa na upande wa mashtaka juu ya ushahidi aliouwasilisha mahakamani hapo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba.
Wakili Nchimbi, ameieleza mahakama kuwa upande wa serikali upo tayari kuendelea kwa usikilizwaji wa shauri hilo.
Wakili Dickson Matata, anayewakilisha upande wa mashtaka ameieleza mahakama kuwa mawakili watatu kwenye safu ya utetezi akiwamo muongoza jopo, Prof. Safari, Kibatala na Mwasipu, wapo kwenye mahakama tofauti kwenye mashauri mengine na kwamba ameitaka mahakama hiyo kuzipangia tarehe nyingine.
Wakili Nchimbi amedai kuwa mawakili hao hawajatoa hati wito wa mahakama na kwamba shauri hilo liliitwa wiki iliyopita na wao walikuwepo mahakamani lakini hawakuiarifu mahakama.
Baada ya kusikiliza pande zote Hakimu ameahirisha kesi hiyo mpaka tarehe 15 Novemba, mwaka huu.
Leave a comment