MAHAKAMA Kuu, Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, Dar es Salaam, imekubali ombi la mawakili wa utetezi katika kesi inayomkabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake, la kujigawa katikati ya usikilizwaji wa kesi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi hilo limekubaliwa Leo Ijumaa, tarehe 17 Septemba 2021, na mahakama hiyo mbele ya Jaji Siyani baada ya kiongozi wa Jopo la mawakili wa utetezi katika kesi hiyo, Peter Kibatala, kuiomba mahakama hiyo ikubali wajigawe.
Awali, Wakili Kibatala, amedai kwamba wameamua kujigawa baada ya kubaini maelezo ya onyo ya mshtakiwa wa pili, Adam Kasekwa yana mgongano wa kimaslahi, akidai yalikuwa yanaelekea kuwataja washtakiwa wenzake.
Wakili Kibatala alidai makamani hapo kuwa, awali mawakili upande wa utetezi walikuwa wanawakilisha washtakiwa wote wanne pamoja, hivyo sasa wanaiomba mahakama hiyo ikubali mawakili hao wajigawe.
Ambapo, Wakili Kibatala alidai, Wakili Nashon Nkungu, atamuwakilisha mshtakiwa wa kwanza, Halfan Hassan Bwire, wakati John Malya atamuwakilisha mshtakiwa wa pili, Kasekwa, huku Dickson Matata, atamuwakilisha mshtakiwa wa tatu, Mohammed Abdillah Ling’wenya.
Jaji Siyani alikubali ombi hilo akisema halitaathiri haki ya mshtakiwa wa pili, kwa kuwa tangu usikilizwaji wa kesi hiyo aliwakilishwa na jopo la mawakili wa utetezi.
Baada ya uamuzi huo, Jaji Siyani alimuita shahidi wa pili wa jamhiri, aliyekuwa Msaidizi wa Mkuu wa upelelezi Arusha Inspekta Mahita Omary Mahita, aanze kutoa ushahidi.
Leave a comment