PENDEKEZO la Tundu Lissu, aliyekuwa Rais wa Chama cha Mawakili wa Tanganyika (TLS) kwamba, Dk. Rugemeleza Nshala anafaa kuwa rais wa chama hicho, limetekelezwa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Wajumbe wa TLS jana tarehe 6 Aprili 2019, wamemchagua Dk. Nshala kuwa rais wa chama hicho kwa mwaka mmoja.
Dk. Nshalla amepokea uongozi huo kutoka kwa rais aliyemaliza muda wake, Fatma Karume ambaye aliyehudumu chama hicho kwa mwaka mmoja.
Kabla ya uchaguzi huo, Lissu aliandika kwenye mtandao wa kijamii kwamba, Dk. Nshalla ndio mtu sahihi baada ya Karume.
Katika uchaguzi uliofanyika jana, Dk. Nshala alipata kura 647 kati ya kura zote 1,227 zilizopigwa.
Uchaguzi huo ulifanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC).
Bahame Nyanduga, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, alitaja wagombea wengine katika nafasi ya urais kwamba, walikuwa John Sekka aliyepata kura 29, Gasper Nicodemus kura 58, Godfrey Wasonga kura 123, Godwin Ngwilimi kura 354.
Akizungumza mara baada ya kutangazwa Rais mpya wa TLS Dk. Nshala, alisema ataendelea kupigania utawala wa sheria na kutekeleza matakwa ya TLS.
Pia TLS itaendelea kuhakikisha wanachama wake wanapata mafunzo mazuri ya sheria.
Leave a comment