MAWAKILI wa pande zote mbili wa kesi zinazowakabili Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake wamekutana na Hakimu Mkazi, Wilbard Mashauri kujua hatma ya watuhumia hao kutofika mahakamani mpaka sasa. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mbowe na viongozi wengine watano walitarajiwa kufikishwa mahakamani leo asubuhi ili kutolewa maamuzi juu ya dhamana yao ikiwa pamoja na kupangwa tarehe ya kuanza kusikilishwa mashtaka yao yanayowakabili, lakini mpaka mchana walikuwa hawajafikishwa mahakamani hapo.
Pamoja na Mbowe, viongozi wengine ni Katibu Mkuu wa chama hicho, Vincent Mashinji, Naibu Katibu Mkuu Bara, John Mnyika, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Salum Mwalimu, Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa na Mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko
Baada ya kutokea mkanganyiko juu ya kutofikishwa mahakamani kwa viongozi hao sita wa Chadema, mawakili wa upande wa mashtaka na wale wanaowatetea watuhumiwa, walilazimika kumfuata hakimu anayesikiliza kesi hiyo, ambaye ametoa ahadi ya kutoa maamuzi muda mchache ujao.
Mawakili wa pande zote mbili wamekubaliano na mahakama, kuwasiliana na Magereza ili kujua sababu ya kushindwa kuwafikisha mahakamani watuhumiwa hao na kujua kama wanaletwa leo au hawaletwi, au mahakama iendeleea kusoma uamuzi wa dhamana hiyo.
Pande zote mbili zimekubaliana kukutana baada ya kufanya mawasiliano hayo ili kupata mrejesho na kujua hatua gani zinafuatwa.
Mahakamani hapo kulifurika umati wa watu wengi wakiwemo wafuasi wa Chadema waliokuwa na kiu ya kusikiliza kesi ya viongozi wao, hali iliyosababisha ulinzi kuimarishwa huku wakiwazuia wafuasi hao kuingia mahakamani.
baadhi ya viongozi wa Chadema waliofika mahakamani hapo ni pamoja na Waziri Mkuu wa zamani na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Edward Lowassa na Waziri Mkuu Mstaafu, Fredrick Sumaye, pamoja na wabunge na madiwani wa chama hicho.
Kutokana na kuchelewa kwa watuhumiwa hao kuwasilishwa mahakamani hapo baadhi ya viongozi walilazimika kuondoka ambapo Lowassa na Sumaye walielekea katika mazishi ya mmoja wa waasisi wa chama hicho, Victor Kimesera, wakati wabunge na madiwani wakielekea ofisi za Umoja wa Ulaya.
Leave a comment