SERIKALI ya Tanzania, imesema imeshindwa kusaini Mkataba wa Umoja wa Afrika (AU) unaohusu masuala ya uchaguzi, demokrasia na utawala bora (ACDEC), kwa kuwa kuna baadhi ya vipengele vinakiuka katiba ya nchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo ilitolewa jana Jumatano, tarehe 8 Desemba 2021 na Mkurugenzi wa Haki za Binadamu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Nkasori Sarakikya, katika mdahalo wa kujadili hali ya haki za binadamu Tanzania, katika kipindi cha miaka 60 ya uhuru wa Tanzania Bara.
Sarakikya alitoa kauli hiyo baada ya mshiriki Abilaly Lugome, kutoka Shirika la Tunaweza, jijini Arusha, kuhoji kwa nini Serikali haijasaini mkataba huo, tangu Umoja wa Afrika (AU), chini ya aliyekuwa Mwenyekiti wake, Rais wa mstaafu wa Tanzania, Jakaya Kikwete, kuuazimia 2007.
Mkurugenzi huyo wa Idara ya Haki za Binadamu, alisema mkataba huo umeweka sharti la matokeo ya urais kupingwa mahakamani, jambo ambalo ni kinyume na katiba ya Tanzania.
“Suala kubwa kwenye huo mkataba ni kwamba unaweza ku-challenge (kupinga) uteuzi wa rais na sisi katiba yetu haituruhusu, kwa hiyo hii challenge ni kubwa kwetu, na ukisema usaini with reservation (uache baadhi ya vipengele) bado kuna obligations (mapingamizi),” alisema Sarakikya.
Sarakikya alisema, kama masharti ya mkataba huo yangekuwa yanaruhusu kukiacha kipengele hicho, Tanzania ingeusaini, lakini fursa hiyo haipo.
“Sababu lazima uiongelee hiyo aspect uliyoiwekea reservation, sasa hiyo reservation ndiyo mkataba wenyewe, kuna mikataba mingine unaweza ku-resave specific aspect lakini huu umenda moja kwa moja lazima uingolee hiyo aspect na reservation ndiyo mkataba wenyewe,” alisema Sarakikya.
Awali, Lugome alihoji kwa nini Tanzania haijasaini mkataba huo, unaochagiza ukuaji wa demokrasia, uchaguzi huru, matokeo ya urais kupingwa mahakamani na uwepo wa tume huru ya uchaguzi.
“Mwaka 2007 Rais Mstaafu Jakaya Kikwete alikuwa Mwenyekiti wa AU, same year akiwa ana-chair kikao waliazimia Umoja wa Afrika kupitisha mkataba huo na yeye akiwa mwenykiti, huu mkataba una vipengele vinaongelea tume huru ya uchaguzi, suala la kuhoji matokeo ya uchaguzi, pia suala la mgombea binafsi,” alisema Lugome na kuongeza:
“Lakini mpaka leo hii Serikali ya Tanzania haijasaini huu mkataba, kama Serikali wana mtazamo gani juu ya huu mkataba na kitu gani kinapelekea wasisaini mpaka leo? Kama wanaona kipengele cha kuhoji matokeo ni interest ya kisiasa kwa nini isisaini with reservation?”
Leave a comment