MATUMAINI ya Erick Kabendera, mwandishi wa habari wa kimataifa wa Tanzania anayeshitakiwa kwa madai ya uhujumu uchumi, kuungana na familia yake yamewekwa njia panda. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya Hakimu Mkazi Mkuu Janet Mtega anayeskiliza shauri lake kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kutofika mahakamani leo, siku ambayo ilitatajiwa hatima ya mazungumzo yake na Mkurugenzi wa Mashtaka ingejulikana.
Aliyetoa taarifa ya kutokuwepo kwa Hakimu Janet alikuwa Mwanasheria wa Serikali Mwandamizi Wankyo Simon akiieleza mahakama kuwa shauri limekuja kwa kutajwa.
Mwanasheria Wankyo alimweleza Hakimu Mkazi Vicky Mwaikambo kuwa Hakimu Janet ameshindwa kufika na akaomba shauri kuahirishwa mpaka siku nyingine.
Hata hivyo haikuelezwa mahakamani sababu ya Hakimu Janet kutofika au amepatwa na dharura gani.
Tarehe 11 Februari 2020, mbele ya Hakimu Janet, mahakama ilielezwa na Wakili wa Serikali Mkuu Faraja Nxhimbi kuwa upande wa mashitaka unaomba kuzungumza na mshitakiwa mwenyewe kuhusu suala la kukiri makosa yake.
Kabendera ambaye alifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza tarehe 5 Agosti 2019 akituhumiwa kwa makosa matatu, likiwemo pia la utakatishaji fedha, alifika mahakamani na kuonekana mtulivu.
Hakimu Mwaikambo aliahirisha kesi mpaka tarehe 24 Februari 2020. Amerudishwa rumande.
Katika kesi hiyo, Kabendera anakabiliwa na kesi ya utakatishaji wa Sh. 173 mil, kujihusisha na mtandao wa kihalifu kwa kutoa msaada kwa genge la uhalifu kwa nia ya kujipatia faida.
Pia inadaiwa Kabendera alitakatisha Sh 173,247047.02, huku akijua fedha hizo ni mazalia ya kosa la kujihusisha na genge la uhalifu na ukwepaji kodi.
Leave a comment