IDRIS Sultan, msanii wa vichekesho na mwenzake Innocent Maiga, wamepandishwa kizimbani kujibu tuhuma za makosa ya mtandaoni. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Wawili hao wamefikishwa mbele ya Rashid Chaungukatika, Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini humo.
Katika shtaka la kwanza, Idriss anadaiwa kushindwa kufanya usajili wa laini ya simu ambayo ilikuwa inamilikwa na mtu mwingine na Maiga anakabiliwa na kosa la kushindwa kutoa taarifa juu ya mabadiliko ya laini ya simu.
Katika shtaka la pili, imedaiwa siku na mahali hapo mshtakiwa Maiga akiwa mmiliki wa laini hiyo ya simu, alishindwa kutoa taarifa ya mabadiliko ya umiliki wa laini hiyo inayotumiwa na Idriss kwa mtoa leseni.
Akisoma mashtaka hayo, Wankyo Simom wakili wa serikali mwandamizi akisaidiana na mawakili wa serikali Batlida Mushi na Estazia Wilson, amedai washtakiwa walitenda makosa hayo katika nyakati tofauti kati ya Desemba Mosi mwaka jana na tarehe 19 Mei 2020, Mbezi Beach ndani ya Wilaya ya Kinondoni.
Washtakiwa wamekana kutenda makosa hayo na wameachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya dhamana, walitakiwa kila mmoja kuwa na wadhamini wawili wenye barua za utambulisho na kusaini bondi ya Shilingi 15 milioni kila mmoja.
Upande wa mashtaka umeieleza mahakama, upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.
Hakimu Chaungu ameahirisha shauri hilo mpaka tarehe 9 Juni 2020, kwa ajili ya washtakiwa kusomewa na imeahirishwa hadi Juni 9 mwaka huu kwa ajili ya maelezo ya awali tayari kwa kuanza usikilizwaji wa kesi.
Washtakiwa hao wanatetewa na wakili Gebra Kambole baada ya wakili Benedict Ishabakaki kuondolewa kuwakilisha washtakiwa kwa sababu atatumika kama shahidi wa upande wa Jamhuri kwa sababu alishuhudia washitakiwa akichukuliwa maelezo ya onyo Polisi.
Wakili Wankyo amedai wakili Ishabakaki hawezi kuendelea na uwakilishi huku pia akiwa ni shahidi wa Jamuhuri tunaomba asiwe kuruhusiwa kuendelea na uwakilishi.
Leave a comment