MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam imebatilisha kifungu cha sheria cha 7(3), kinayowaruhusu Wakurugenzi wa Manispaa na Halmashauri kuwa wasimamizi wa Uchaguzi nchini. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Leo tarehe 10 Mei, 2019, uamuzi huo umetolewa na Jaji Utuganile Ngwala katika kesi namba 8 ya mwaka 2018, iliyofunguliwa na Bob Chacha Wangwe, Mwanachama wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Katika maamuzi hayo, Jaji Ngwala pia ametengua kifungu cha 7 (1) kinachoruhusu mtu yeyote kuwa msimamizi wa uchaguzi.
Jaji Ngwala akisoma uamuzi huo, amesema kuwa sheria hizo ni batili na kinyume cha katiba ya nchi.
Amesema kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa kwenye mahakama hiyo na muombaji kuwa wasimamizi wa chaguzi ni wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambao wanamaslahi kwenye chaguzi hizo.
Muombaji (Bob) amewakilishwa na Wakili Fatma Karume, kwenye kesi hiyo ambaye ametoa ushahidi wa majina 74 ya wasimamizi wa uchaguzi ambao ni wanachama wa (CCM).
Jaji Ngwala amesema kuwa sheria hizo hazijaelekeza utaratibu wowote wa kuhakiki kuwa wasimimizi hawana maslahi binafsi na uchaguzi.
Amesema ya kuwa sheria hii ya Tume ya Uchaguzi imekataza mtu yoyote ambaye mwanachama wa chama chochote haruhusiwi kuwa msimamizi wa Uchaguzi.
Leave a comment