WAZIRI wa Fedha na Mipango wa Tanzania, Dk. Mwigulu Nchemba, amependekeza marekebisho ya Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani ili kurudisha utaratibu wa kurejesha VAT kwa bidhaa zinazonunuliwa Tanzania Bara na kutumika Tanzania Zanzibar. Anaripoti Jemima Samwel, DMC…(endelea).
Akiwasilisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2021/22, leo Alhamis bungeni jijini Dodoma, Dk. Mwigulu amesema, hii inatokana na mfumo wa kutoza VAT kwa kiwango cha asilimia sifuri kwa bidhaa za viwandani pekee kutowanufaisha wafanyabiashara wa Zanzibar wanaonunua bidhaa na kutozwa VAT Tanzania Bara na kutozwa tena VAT bidhaa hizo zinapopelekwa Zanzibar.
“Aidha, inapendekezwa marejesho ya VAT yatakayofanyika kwa bidhaa zinazotoka Tanzania Bara kwenda Zanzibar yafanyike pia kwa bidhaa zitakazotoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara sambamba na marekebisho ya vifungu husika vya Sheria za VAT kwa pande zote mbili za muungano.”
“Ili kuwa na ufanisi wa marejesho, maboresho ya mifumo yatafanyika ili isomane baina ya Tanzania Bara na Zanzibar,” amesema Dk. Mwigulu na kuongeza:
“Kutokana na utaratibu huu, kiwango cha asilimia sifuri ya Kodi ya Ongezeko la Thamani kilichokuwa kinatozwa bidhaa hizo kitasitishwa.”
Leave a comment