WADAU wa tasnia ya habari Tanzania, wameshauri mchakato wa marekebisho ya sheria zinazosimamia vyombo vya habari, ukamilike ili kukidhi dhamira ya Rais Samia Suluhu, katika kuimarisha uhuru wake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ushauri huo umetolewa leo Alhamisi, tarehe 20 Oktoba 2022, katika mkutano wa kujadili sheria za habari, uliondaliwa na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) na kufanyika jijini Dar es Salaam.
Mjumbe wa Kamati Kuu ya TEF, Salim S. Salim, amesema kauli zinazotolewa na Rais Samia kuhusu uimarishaji uhuru wa vyombo vya habari ni nzuri lakini haziwezi kuleta tija iwapo marekebisho ya sheria hayatafanyika.
“Kauli za Rais Samia ni nzuri, lakini sio sheria inabidi tuhakikishe marekebisho ya sharia yanafanyika ili tuwe na sheria nzuri,” amesema Salim.
Naye aliyekuwa Mwenyekiti wa TEF, Theophil Makunga amesema uongozi wa Serikali ya Rais Samia umeonesha dhamira njema ya kuboresha tasnia ya habari, na kuwataka wadau wake kuitumia fursa hiyo vizuri.
“Angalia waziri ambaye sasa hivi anasimulia mabadiliko (Nape Nnauye) ndiyo huyu alikuwa anasimamia sheria hiyo, sasa amebadilikaje? ni kutokana na political will iliyokuwepo,” amesema Makunga.
Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile, ameipongeza Serikali kwa kuyachukua moja kwa moja baadhi ya mapendekezo ya wadau kuhusu marekebisho ya vifungu kandamizi vya Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari ya 2016.
Pia akiiomba Serikali imalizie kuyachukua mapendekezo mengine yaliyosalia, ambayo inaendelea kuyafanyia kazi.
Kwa mujibu wa Balile, Serikali imechukua moja kwa moja mapendekezo ya wadau kuhusu marekebisho ya vifungu zaidi ya 10 vya sheria hiyo, ikiwemo cha 38, 50, 52, 53, 54, 55, 56 na 57.
Vifungu hivyo vinahusu masuala ya makosa ya uchochezi, utoaji adhabu kwa wamiliki wa viwanda vya uchapishaji magazeti endapo vitachapisha habari za uchochezi, mamlaka ya waziri mwenye dhamana ya habari kuamua aina ya maudhui yanayochapishwa na vyombo vya habari.
“Kuanzia kifungu cha 38 hadi 57, mapendekezo hayo Serikali imeyachukua neno kwa neno lakini sababu hayajaingia bungeni huwezi kusema yamechukuliwa lakini tunasema yachukuliwe,” amesema Balile.
Mwenyekiti huyo wa TEF, ametaja baadhi ya mapendekezo ya wadau ambayo Serikali inaendelea kuyafanyia kazi, kuhusu marekebisho ya vifungu vya sheria hivyo takribani 20.
Miongoni mwa vifungu hivyo ni, 3,5,7,9 na Cha 11 hadi 23, 35, 36 na 37.
Vifungu hivyo vinahusu tafsiri na utambuzi wa mwandishi wa habari, usajili wa magazeti, uratibu wa matangazo ya Serikali, mamlaka ya Serikali kuongoza vyombo vya habari maudhui ya kuchapisha au kutangaza na Mamlaka ya Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo, kukataa maombi, kusitisha au kufuta leseni ya magazeti.
Leave a comment