UBALOZI wa Marekani nchini Tanzania, umeleza kuwepo mipango ya matukio ya mashambulizi kwenye hoteli na migahawa jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kutokana na kitisho hicho, ubalozi huo umetoa tahadhari kwa raia wake waishio hapa nchini kwa kuwataka kuwa makini.
Taarifa hiyo iliyotolewa leo tarehe 19 Juni 2019 imeeleza kuwa, maeneo yaliyolengwa ni kwenye hoteli na migahawa ya kitalii iliyopo Masaki.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa, ubalozi huo umepata tetesi za uwepo wa tishio la kiusalama katika maeneo hayo na kwamba, maeneo lengwa ni yale wanayopenda kutembelewa na watalii pamoja na Duka la Kisasa la Slipway Shopping Center.
Aidha, Ubalozi wa Marekani umesema, hauna uhakika wa kipindi ama muda ambao tukio hilo limepangwa kutokea.
Kufuatia tetesi hizo, imewataka raia wake kuwa na tahadhari.
Ubalozi huo umetoa wito kwa raia wake kuwa makini na maeneo waliyopo, pia maeneo ya kitalii na yanayopendwa na raia wa kigeni, pamoja na kufuatilia taarifa za vyombo vya habari.
MwanaHALISI ONLINE ilimtafuta Kamamda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa kwa njia ya simu kwa ajili ya ufafanuzi wa taarifa hiyo, lakini simu yake kuita bila kupokewa kisha kutokuwa hewani.
Leave a comment