MAKAMU wa Rais wa Marekani, Kamala Harris amesema miongoni mwa msururu wa hatua mpya za kuimarisha uhusiano wa kiuchumi na Tanzania, Benki ya EXIM ya Marekani itasaini hati ya makubaliano (MoU), kuwezesha kampuni za Marekani kupeleka bidhaa na huduma nchini Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kamala ametoa ahadi hiyo leo Alhamisi tarehe 30 Machi 2023, wakati akizungumza mbele ya waandishi wa habari Ikulu jijini Dar es Salaam muda mfupi baada ya kupokewa na mwenyeji wake Rais Samia Suluhu Hassan.
Msaidizi huyo wa Rais Joseph Biden yupo ziarani nchini Tanznaia ikiwa ni miongoni mwa nchi tatu anazozitembelea kwa siku tisa, ikiwa n a lengo la kuimarisha uhusiano na nchi hizo katika masuala ya kiuchumi, usalama wa chakula, afya na wanawake, mazingira na mabadiliko ya tabia ya nchi.
Hati hiyo ya makubaliano ambayo itawezesha upatikanaji wa hadi Dola za Kimarekani milioni 500 kugharimia upelekaji wa huduma na bidhaa (export financing) Tanzania, itasaidia upelekaji wa bidhaa na huduma hizo katika sekta mbalimbali hususan, miundombinu, usafirishaji, teknolojia ya kidijitali, nishati na miradi ya nishati jadidifu.
Kamala amesema, kwa kuimarisha na kuongeza fursa za kiuchumi, makubaliano hayo yatasaidia kukuza ajira nchini Tanzania na Marekani.
“Aidha, makubaliano haya yanathibitisha azma ya dhati ya Serikali ya Marekani ya kuhuisha ubia na ushirikiano na Afrika na kujenga dhima rasmi ambayo EXIM imepewa na Bunge la Marekani ya kuongeza na kuimarisha uhusiano kati ya wafanyabiashara wa Kimarekani wanaouza bidhaa na huduma nje ya Marekani (exporters) na nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara,” amesema Kamala.
Mbali na hayo hatua mpya zingine za kuimarisha uhusiano wa kiuchumi baina ya nchi hizo ni pamoja na kuzinduliwa kwa Majadiliano ya Kibiashara kati ya Marekani na Tanzania ambapo Wizara ya Biashara na Viwanda ya Tanzania na Wizara ya Biashara ya Marekani zinatarajia kusaini Hati ya Makubaliano (MOU) kuanzisha majadiliano rasmi ya kibiashara baina ya nchi mbili.
Pia Marekani itatoa huduma za ushauri wa kitaalamu kwa Serikali ya Tanzania. Programu ya Tanzania ya Huduma ya Ushauri kuhusu Uendeshaji na Biashara ya Bandari inalenga kusaidia jitihada za Serikali ya Tanzania kutumia kikamilifu fursa za uwekezaji na kuvutia wawekezaji wa aina mbalimbali
Leave a comment