AHADI ya Rais John Magufuli kwamba, atahakikisha uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka huu unakuwa huru na haki, imeungwa mkono na Marekani. Anaripoti Martin Kamote, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa ya Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania iliyotolewa leo tarehe 31 Januari 2020, imeeleza kufurahishwa na ahadi ya Rais Magufuli aliyoitoa tarehe 21 Januari 2020 kwamba, uchaguzi huo hautafinyangwa.
“Mwaka 2020 mwezi Oktoba, nchi yetu itafanya uchaguzi mkuu, zoezi la uchaguzi ni muhimu kwa nchi yoyote inayofuata misingi demokrasia, Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa uchaguzi mkuu unafanyika katika mazingira ya amani, uhuru na haki” alisema Rais Magufuli.
Alitoa kauli hiyo alipokutana na mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao Tanzania wenye sherehe za mwaka mpya 2020 na chakula cha jioni Ikulu, Dar es Salaam.
Taarifa ya ubalozi huo imeeleza “tumetiwa moyo sana na hakikisho lililotolewa na Raisi Magufuli hapo tarehe 21 Januari 2020, kwamba uchaguzi mkuu wa mwaka 2020, utakuwa huru, haki na uwazi pamoja na mwaliko wake kwa waangalizi wa uchaguzi wa kimataifa.
“Tunatarajia uchaguzi ambao raia wote na wagombea wa vyama vyote, wanaweza kukutana kwa amani, wakieleza mawazo yao na kampeni zitakazofanyika katika misingi ya usawa.”
Hata hivyo, Ubalozi umetoa wito kuhakikishiwa zoezi la uandikishaji wapiga kura lenye uwazi, kuanzishwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi na kuteuliwa mapema kwa waangalizi wa uchaguzi wa kitaifa na kimataifa wa kuaminika, na watakaofuatilia uchaguzi kwa kipindi kirefu na kifupi.
Leave a comment