SEKRETARIETI ya Shirikisho la Mpira wa miguu Tanzania (TFF) imewafungulia mashtaka ya kimaadili Rais wa Yanga Mhandisi Hersi Said na aliyekuwa Msemaji wa klabu hiyo, Haji Manara. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya Manara anayetumikia kifungo cha kukaa nje miaka miwili bila kujishughulisha na shughuli yoyote ya mpira wa miguu, alichoadhibiwa na kamati ya maadili TFF, kupanda jukwaani katika kilele cha Siku ya Wananchi na kutambulisha wachezaji, benchi la ufundi na viongozi.
Hata hivyo, mwisho wa utambulisho huo, aliwaeleza umati wa wananchi waliokuwa wamehudhuria hafla hiyo katika uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam kuwa aliifanya kazi hiyo kama MC mwalikwa na hahusiki na mambo ya soka kabisa.
Manara alisema; “Nipo hapa kama walivyoalikwa kina Zembwela, Dakota na Maulid Kitenge, nimemaliza kazi yangu naondoka kabisa uwanjani kwenda kwenye kazi ya UMC Kidogo.”
Aidha, leo tarehe 7 Agosti, 2022, Ofisa Habari na Mawasiliano wa shirikisho hilo, Cliford Ndimbo ametoa taarifa kwa umma kwamba Manara ameshindwa kutekeleza adhabu hiyo.
Pia Mhandisi Said amefunguliwa mashtaka kwa kwenda kinyume na ibara ya 16(1)a ya Katiba ya TFF pamoja na ibara ya 1(6) ya katiba ya Yanga.
“Baada ya Manara kuadhibiwa na Kamati ya Maadili TFF, Sekretarieti ilimwandikia barua Mhandisi Said kuhakikisha klabu yake inaheshimu uamuzi huo.
“Mwenyekiti wa kamati ya maadili TFF tayari amepelekewa mashtak hayo, walalamikiwa watapewa mashtaka na mwito mara baada ya kamati hiyo kupanga tarehe ya kusikiliza mashtaka hayo,” imesema taarifa hiyo.
Asante sana hapa duniani hakuna kibari cha kudharu mamlaka na anayezarau mamlaka atambue amejidharaulisha