Afisa Habari wa klabu ya Simba Haji Manara amemtaka beki wa kushoto wa Timu hiyo Mohammed Hussein kuongeza mkataba kutokana na uwezo wake mkubwa aliouonesha akiwa na kikosi hiko. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Mkataba wa mchezaji huo unaenda kuisha mwishoni mwa msimu huu wa 2020/21 ambapo alisaini kwa miaka miwili.
Manara ameyasema hayo kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa kijamii wa Instagram mara baada ya mchezaji huyo kufunga bao pekee kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Gwambina FC.
Msemaji huyo aliandika kuwa wanasimba wanataka mchezaji amalizane na uongozi kuhusu usajili wake kwa kuwa hawako tayari kumpoteza na kumtaka mtendaji mkuu wa klabu hiyo Barbara Gonzalez kulisimamia suala hilo kwa kuwa wanasimba hawato waelewa.
“Wanasimba wamenituma nikwambie hadharani,,umalizane haraka na uongozi wa klabu kuhusu usajili wako na hawatakubali kukupoteza kwa namna yoyote ile.. sanasana watakuruhusu uende nje ya nchi hii,sio vtimu vya ajabu ajabu visivyojua kesho yao”
“Barbara boss wangu, nchi haitatuelewa Zimbwe akiondoka kwenda timu za hovyo hovyo, Huyu ni Mtoto wa Simba, limalize hili tuendelee kuonyesha nini Simba inadhamiria katika muendelezo wa ukubwa wake!!” aliandika Haji
Andiko la msema huyo limekuja kufuatia tetesi za kuwa klabu ya Yanga ipo katika mazungumzo na mchezaji huyo aliyedumu kwenye kikosi cha Simba kwa miaka saba.
Mara baada ya Manara kuandika hayo, msemaji wa klabu ya Yanga Antonio Nugaz alimjibu kwa kusema kuwa wamuombe dua njema na wamuache afanye maamuzi yake yeye mwenyewe.
“Muombee Dua njema na Acha afanye Maamuzi yake yenye Tabasamu endelevu” alijibu Nugaz
Mchezaji huyo ambaye ni nahodha msaidizi alijiunga na klabu ya Simba mwaka 2014 akitokea klabu ya Kagera Sugar.
Leave a comment