MAMIA ya watu wameuaga mwili wa aliyekuwa mwandishi na mchambuzi wa masuala ya kisiasa nchini Tanzania, Padri Privatus Karugendo (65). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Mwili huo umetolewa heshima za mwisho leo Jumatatu tarehe 28 Juni 2021, kwenye ibada iliyofanyika katika Kanisa Katoliki la Roho Mtakatifu Segerea, jijini Dar es Salaam.
Padri Karugendo alifariki dunia usiku wa kuamkia tarehe 24 Juni 2021, katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, alikokuwa anapatiwa matibabu baada ya kuugua kwa muda mfupi.
Miongoni mwa watu walioshiriki ibada hiyo ni aliyekuwa Mkurugenzi wa Bohari Kuu ya Dawa (MSD), Laurian Bwanakunu na Jennifer John, mke wa Innocent Nashungwa ambaye ni Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo pia waziri wa zamani wa ardhi, Anna Tibaijuka.
Akizungumza katika ibada hiyo, amesema kifo cha Padri Privatus kimeacha pigo, kwa kuwa alikuwa mtu muhimu katika familia yake na Taifa kwa ujumla.
“Kupitia kalamu yake, aliweza kutoa maoni ya watu wengi. Alikuwa mwenye hekima na busara, hakuchukia mtu hata kama ulikuwa unatofautiana naye kimtazamo ama maoni,” amesema Jeniffer.
Akisoma wasifu wa Padri Karugendo, Msemaji wa Familia, Emillianus Karugendo amesema alizaliwa tarehe 14 Januari 1956, Bukoba Vijijini mkoani Kagera.
Emillianus amesema, Padri Karugendo ameacha mjane, Rose Birusya na mtoto mmoja, Yesigwe Karugendo.
Baada ya mwili huo kutolewa heshima za mwisho, ulisafirishwa kuelekea makaburi ya Kinondoni mkoani Dar es Salaam, kwa ajili ya mazishi.
Enzi za uhai wake, alikuwa Padri kwa miaka takribani 20 ikiwemo katika Jimbo Katoliki la Rulenge, Parokia ya Buziku mkoani Kagera, alikokuwa Paroko Msaidizi.
Pia alikuwa mwandishi na mchambuzi wa siasa katika gazeti la Mwananchi na Idhaa ya Kiswahili ya Ujerumani, Deutsche Welle.
Mwaka 2009, Padri Karugendo alivuliwa upadri kwa tuhuma za kukiuka maadili ya Kanisa Katoliki.
Mgogoro wa Padri Karugendo na kanisa hilo ulianza kufuatia msimamo wake wa kuunga mkono matumizi ya Kondomu, kwa ajili ya kujikinga maambukizi ya Virusi vya Upungufu wa Kinga Mwilini (Ukimwi).
Miaka minane baadaye tarehe 26 Aprili 2017, alifunga ndoa na mchumba wake Rose Birusya, jijini Dar es Salaam.
Leave a comment