MAKAMU Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) – Bara, Tundu Lissu amewasili rasmi nchini Tanzania leo Jumatano tarehe 25 Januari 2023 akitokea nchini Ubelgiji na kulakiwa na mamia ya wanachama na Watanzania waliojitokeza kumpokea. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar….(endelea)
Lissu amewasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere na ndege ya Shirika la Ndege la Ethiopian Airways saa 7.05 mchana na kulakiwa na mamia ya wanachama na wapenzi wa chama hicho nje ya uwanja huo.
Lissu ambaye alikuwa mgombea Urais kwa tiketi ya Chadema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020, amepokewa kwa shangwe na vikundi vya ngoma na bodaboda ambazo zimepambwa kwa bendera ambazo zinaongoza msafara wake kutoka uwanjani hapo kuelekea katika uwanja wa Buriaga – Temeke ambako atakuwa na mkutano.
Jeshi la Polisi limeimarisha ulinzi na kuhakikisha wafuasi na wapenzi hao wa Chadema hawaingii ndani ya uwanja wa ndege ili kuruhusu huduma zingine kuendelea bila usumbufu.
Pia wamesindikiza msafara wa Lissu ambao una msururu mrefu wa magari, bodaboda na wengine wanaotembea kwa miguu.
Leave a comment