JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limesema litawashughulikia kisheria wale wote wenye lengo la kufanya vurugu siku ya uchaguzi mdogo wa Ubunge utakaofanyika tarehe 16 Septemba 2018 katika Jimbo la Ukonga na udiwani katika Kata ya Vingunguti. Anaripoti Khalifa Abdallah … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema kuwa jeshi hilo limejiandaa vizuri kusimamia ulinzi na usalama wa raia katika siku hiyo na kuwa kila kituo cha kupiga kura kutakuwa na askari wa vikosi mbalimbali wakifanya doria kila sehemu huku wakiongozwa na askari maalum wa kikosi cha kutuliza ghasia.
“Jeshi halitasita kuchukua hatua za haraka za kisheria kwa mtu yeyote au kikundi cha watu wenye nia ya kufanya vitendo vyovyote ambavyo ni kinyume na kanuni au sheria ya uchaguzi,” amesema.
Mambosasa amesema kuwa wananchi waishio katika jimbo la Ukonga wasiwe na hofu yoyote kwakuwa waliopanga kufanya vurugu watashughulikiwa kwa mujibu wa sheria.
“Polisi wataendelea kusimamia hadi utoaji wa matokeo ili asitokee mtu akataka kufanya ndivyo sivyo, kuna watu wamekuwa na tabia wakipiga kura wanang’ang’ania sehemu hizo za kupigia kura kwa lengo la kuja kufany vurugu, kwa namna ambavyo tumejipanga atakayejaribu kufanya atakalo ataishia kwenye vituo vya Polisi,” amesema.
Leave a comment