LAZARO Mambosasa, Kamanda wa Jeshi la Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, amewataka watu wanaosambaza taarifa, kwamba Rais John Magufuli mgonjwa, waache. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akijibu swali la waandishi wa habari leo Jumatano, tarehe 17 Machi 2021, jijini Dar es Salaam kuhusu watu wanaokamatwa kutokana na kile kilichodaiwa, kutoa taarifa za uzushi kwamba Rais Magufuli mgonjwa, amesema mtoa taarifa lazima ajiridhishe.
“Ninachosema kwa Watanzania, waache kuwa wazushi wa kupokea taarifa ambazo hawajazifuatilia wakijua ukweli wake, kuzisambaza na kuendelea kuvumisha uvumi ambao hauna maana,” amesema SACP Mambosasa.
Taarifa kwamba, kiongozi huyo ambaye hajaonekana hadharani kwa zaidi ya siku 17 sasa, zimekuwa zikitawala kwenye mitandao ya kijamii na vyombo vya habari ndani na nje.
Kamanda Mambosasa amewataka wananchi kuacha kusambaza taarifa hizo ambazo hazijathibitishwa ukweli wake.
Hadi sasa watu kadhaa wanashikiliwa na Jeshi la Polisi katika maeneo mbalimbali kwa tuhuma za kusambaza taarifa hizo.
Jumatatu ya tarehe 15 Machi 2021, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassani aliwatoa hofu Watanzania akiwataka kupuuza taarifa hizo, kwa kuwa Rais Magufuli yu bukheri wa afya na anaendelea na majukumu yake.
Leave a comment