KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Antonio Guterres aliwahi kusema; “Ushirikiano wa kimataifa na diplomasia vimethibitisha kuwa na faida na huduma muhimu kwa watu wote duniani kuanzia masuala ya utekelezaji wa sheria za kimataifa, usawa wa kijinsia, ulinzi wa mazingira, hadi kuzuia uzalishaji wa silaha za maangamizi na hata magonjwa hatari duniani.” Anaandika Mwandishi Wetu … (endelea).
Guterres aliongeza kusema ushirikiano wa kimataifa na diplomasia ni kwa ajili ya amani, na utulivu huo huleta maendeleo kwa taifa husika.
Tarehe 25 Mei 20225, Rais Samia Suluhu Hassan alipewa Tuzo ya Babacar Ndiaye kwa mwaka 2022 ikiwa ni kutambua jitihada anazozifanya katika ujenzi wa miundombinu nchini.
Watu mbalimbali wameendelea kutoa maoni kuhusu namna mwanamama huyu wa kwanza barani Afrika alivyofunika maelfu ya wanasiasa katika kinyang’anyiro hicho kwa mwaka 2022.
Miongoni mwa watu hao ni mchambuzi wa masuala ya siasa na uchumi nchini, Meijo Laiser ambaye anasema kuwa ni dhahiri sasa kuwa vyombo vya habari duniani vinaitaja Tanzania kama sehemu salama katika uendeshaji wa shughuli za kiuchumi na uwekezaji, kisiasa na shughuli za kijamii.
Laizer anaweka bayana masuala mbalimbali ambayo Rais Samia, ambaye alinukuliwa wakati akipewa tuzo hiyo kuwa alistahili mtangulizi wake Dk. John Pombe Magufuli, lakini haina namna.
“Watanzania sote ni mashuhuda katika yote yanayofanyika katika Serikali ya Awamu ya Sita ikiwamo suala la ujenzi wa madarasa kwa kutumia fedha zilizotokana na udhibiti wa Uviko- 19, ni jambo jema na ni dhamira njema,” anasema Laiser.
Laiser anafafanua kuwa Serikali imeendelea kutoa kipaumbele katika huduma za afya zenye ubora na zinazowafikia wananchi wote ili kuboresha afya zao.
“Serikali imekuwa ikitambua umuhimu wa afya bora kwa wananchi wake kwani afya bora ni raslimali muhimu kwa maendeleo ya nchi kwa ujumla,” anabainisha mchambuzi huyo wa masuala ya siasa.
Swali la jinsi ya kutoa elimu yenye ubora limeamsha hisia za wadau wa elimu. Ubora wa elimu unategemea ubora wa kinachoingizwa, mchakato na matokeo yake, ambapo Rais Samia ameonesha namna ubora huo unavyoweza kufikiwa kwa vitendo.
“Utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu imeboreshwa zaidi kwa kuwepo ongezeko kubwa la wanufaika. Yote haya ni kazi nzuri ya Serikali ya awamu ya sita,” anasema Laiser na kuongeza kuwa;
“Uboreshaji katika upatikanaji wa maji kwa maeneo ya vijijini na mijini kwa ujumla ni kazi nzuri inayofanywa katika nchi ya Tanzania, hivyo kupatiwa kwa tuzo hiyo huko Ghana imekua zawadi kubwa kwa Watanzania, hivyo kuna kila sababu ya kumuunga mkono kiongozi mkuu wa nchi.”
Pia anasema uboreshaji wa maslahi ya watumishi wa umma ni miongoni mwa jitihada za Rais Samia ambapo asilimia 23.3 ya mshahara imeongezwa kwa watumishi wa umma.
“Ukusanyaji wa mapato kwa sasa imevuka malengo, wananchi wengi wametambua umuhimu wa kulipa kodi,” anasema.
Aidha, Laiser anasema kuwa, Rais Samia amekuwa mstari wa mbele katika masuala yanayohusu maridhiano hususan ya kisiasa.
Ambapo ameanzisha majadiliano kwa lengo la kupata muafaka wa kisiasa kati ya chama tawala (CCM) na vyama vya upinzani, hatua ambayo imejenga heshima na dhamira njema kwa taifa na watu wake.
Kama ambavyo, Guterres anasisitiza kuhusu ushirikiano baina ya mataifa kwamba lazima kuthibitisha faida zake, na si jambo linalokubalika kuwapuuza wanaotilia mashaka, ni lazima kuonesha kwamba ushirikiano wa kimataifa unaweza kukabiliana na changamoto za kimataifa na kuleta utandawazi wa kimataifa utakaokidhi matakwa ya wote.
Ndivyo ambavyo Rais Samia ameithibitishia dunia kuwa ushirikiano unalipa na wale wanaoubeza wanapaswa kutambua haitafaa kitu katika ujenzi wa taifa la Tanzania.
CCM Kilimanjaro yampongeza
Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mkoa wa Kilimanjaro kimempongeza Rais Samia kwa kutwaa tuzo ya Babacar Ndiaye, kutoka Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB).
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na MwanaHALISI Online katika mahojiano maalum ofisi za chama hicho, Mwenyekiti wa CCM mko huo, Patrick Boisafi, anasema tuzo hiyo ni matokeo ya kazi nzuri inayofanywa na Serikali inayoongozwa na Rais Samia.
“Tuzo hii inatokana na kutambua kazi kubwa ya ujenzi wa miundombinu, iliyofanywa na nchi yetu ya Tanzania ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuifungua Afrika kimaendeleo,” anasema Boisafi.
Anafafanua kwamba; “Kutambulika na pongezi anazopokea Rais Samia kimataifa ni matokeo ya kazi nzuri anayoifanya na Serikali, tumepata Rais mwenye nia, dhamira na malengo ya kuwaletea Watanzania maendeleo,” anasema.
Katibu wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Jonathan Mabihya, anatoa mwito kwa Watanzania kuendelea kumuunga mkono Rais Samia kwa kufanya kazi kwa bidii ili aendelee kufanikisha mambo makubwa kwa Taifa katika kuwaletea maendeleo wananchi.
Leave a comment