USHIRIKIANO kati ya Tundu Lissu, mgombea urais wa Tanzania Bara kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Bernard Membe wa Chama cha ACT-Wazalendo, upo njia panda. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, kuonya kwamba ushirikiano unaohubiriwa na vyama hivyo, unakiuka sheria za uchaguzi.
Taarifa za ushirikiano wa vyama hivyo viwili vya upinzani vyenye nguvu nchini, umeelezwa kufikia hatua za mwisho ambapo tarehe 3 Oktoba 2020 unatarajiawa kuwekwa hadharani.
Hata hivyo, Sisty Nyahoza ambaye ni Naibu Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, amesema muungano wowote wa vyama vya siasa miezi mitatu kabla ya kufikia tarehe ya uchaguzi, ni kinyume cha sheria.
Soma zaidi:-
“Sisi tunasimamia sheria ya vyama vya siasa, na ile sheria katika kifungu cha 11A kimeweka utaratibu ambapo vyama vya siasa viwili au zaidi ya viwili, vikitaka kushirikiana katika masuala ya uchaguzi, kuna utaratibu vinatakiwa vifuate.
“Moja wanatakiwa waitishe mikutano mikuu ya kila chama kimoja kuweza kuamua, pili waingie mkataba wa kushirikiana halafu ule mkataba unatakiwa uletwe kwa msajili wa vyama vya siasa miezi mitatu kabla ya uchaguzi kuanza,” amesema Sisty.
Amesema, vyama hivyo kama vitatangaza kuungana bila kufuata utaratibu huo, vitakuwa vinakiuka sheria ya vyama vya siasa.
Akizungumzia hatua ya Chama cha TLP na UDP kutangaza kumuunga mkono Dk. John Magufuli, mgombea urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) bila kufuata taratibu hizo, Sisty amesema ‘nao wamekosea.’
“Wale walitamka kabla ya uteuzi wa wagombea, lakini ukishaenda jukwaani na kuanza kumnadi mgombea, ina maana ndio ushirikiano wenywe. Katika ushindani, hutakiwi kufanya jambo ambalo litawa-surprise (litawashangaza) wenzako halafu ukasema hii nafuata sheria, hii hapana.
“Kwa mfano TLP ambao wao walisema na kwa bahati mbaya wao baada ya uteuzi wa wagombea, wakaweka mabango ya picha ya mgombea wa TLP na mgombea wa chama kingine, tumewaandikia barua wajieleze, ndio maana na wagombea wengine mfano Chadema, tumemwandikia baraua na ajieleze,” amesema.
Lissu akiwa visiwani Zanzibar kwenye mkutano wake wa kampeni za urais, alimnadi Maalim Seif Sharif Hamad, mgombea urais visiwani humo kupitia Chama cha ACT-Wazalendo kwamba anaungwa mkono na chama chao.

Tayari Maalim Seif amewaeleza Wazanzibari na Watanzania kwamba, chama chake kinamuunga mkono Lissu kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika tarehe 28 Oktoba 2020.
Zitto Kabwe, Kiongozi wa ACT-Wazalendo akiwa mkoani Mtwara hivi karibuni, alimpigia kampeni mgombea udiwani wa Chadema Kata ya Chiungutwa, Frank Masimisia.
Ofisi ya Msajili imeandika barua yenye tarehe 18 Septemba 2020, kwenda kwa makatibu wakuu wa vyama vya siasa, ikieleza kuwa muungano wowote unaoweza kufanywa sasa, unakiuka sheria.
“Katika mikutano ya baadhi ya kampeni ya baadhi ya wagombea wameonekana au kusikika wakiwaombea kura wagombea wa chama cha siasa kingine.
“Kifungu cha 11A cha Sheria ya Vyama vya Siasa Sura ya 258 kimeweka utaratibu wa vyama kushirikiana katika uchaguzi. Vyama vya siasa vikishirikiana bila kufuata utaratibu uliowekwa ni kukiuka sheria,” inaeleza barua ya Nyahoza.
Kwa kujibu wa barua hiyo, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa imeahidi kuvichukulia hatua za kisheria vyama vya siasa vitakavyo kiuka Sheria ya Vyama Vya Siasa na Sheria ya Gharama za Uchaguzi Sura ya 278 katika mikutano ya kampeni.
“Hivyo Msajili wa Vyama vya Siasa anawakumbusha wagombea na vyama vya siasa kuzingatia masharti ya sheria katika kampeni za uchaguzi.
“Mnapaswa kukumbuka pia ni wajibu wa msajili wa vyama vya siasa kuchukua hatua za kisheria pale chama cha siasa kinapokiuka sheria ya vyama vya siasa na Sheria ya Gharama za Uchaguzi Sura ya 278.
“Hivyo msajili wa vyama vya siasa hatasita kuchukua hatua stahiki za kisheria pale itakapothibitika chama cha siasa kimekiuka sheria hizo,” inaeleza barua hiyo.
Akizungumza na mtandao huu, Janeth Rithe ambaye ni Katibu wa Itikadi na Uenezi (ACT-Wazalendo), ameeleza kupokea barua hiyo ya msajili inaeleza onyo la vyama vya saisa kushirikiana na taratibu zake.
Leave a comment