MWANASIASA mkongwe nchini Tanzania, Getrude Mongella, amewataka Watanzania kutokuwa na wasiwasi juu ya uongozi wa Rais wa Awamu ya Sita wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Mama Mongella ametoa wito huo leo Jumatatu tarehe 26 Aprili 2021, wakati akizungumza katika Kongamano la Miaka 57 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, lililofanyika jijini Dodoma.
Muungano huo, ulifanyika tarehe 26 Aprili 1964, chini ya aliyekuwa Rais wa Tanganyika, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na aliyekuwa Rais wa Zanzibar, Hayati Sheikh Abeid Amani Karume
Rais Samia aliapishwa kuwa Rais wa Tanzania tarehe 19 Machi 2021, kufuatia kifo cha aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dk. John Magufuli, kilichotokea kwenye Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam, tarehe 17 Machi 2021.
Akizungumza katika kongamano hilo, Mama Mongella amesema, Rais Samia ana uzoefu wa kutosha katika masuala ya uongozi.
Rais huyo wa zamani wa Bunge la Jumuiya ya Afrika, amesema alifahamu uwezo wa Rais Samia katika Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Masuala ya Wanawake uliofanyika 1995, jijini Beijinga nchini China.
Mongella aliyekuwa Katibu Mkuu wa mkutano huo, amesema kwenye mkutano huo, Rais Samia alishiriki vilivyo kuwasilisha ajenda za wanawake wa Tanzania.
“Tunaye Samia, binti mwenye uwezo wa hali ya juu, namfahamu na alienda mpaka Beijing kutokea ujumbe wa Tanzania, na alisaidia sana katika ujumbe wa Watanzania waliokuja Beijing, kuanzia hapo namfahamu, msiwe na wasiwasi nae,” amesema Mama Mongella.

Mama Mongella amesema, amefurahi kuona Tanzania inaongozwa na mwanamke, kwani ilikuwa kiu yake ya muda mrefu.
“Nimefurahi zaidi kuona ya kwamba katika uhai wangu nchi hii inaongozwa na mwanamke, ni kitu nilianza kukata tamaa pamoja na kuzunguka dunia nzima nikiimba wimbo kwamba wanawake wanaweza. Lakini imewezekana,” amesema Mongella.
Mwanaharakati huyo wa haki za wanawake, amesema Dk. Mgaufuli anastahili kuenziwa kwa uamuzi wake wa kumteua Rais Samia kuwa makamu wake wa rais, hali iliyopelekea mabadiliko ya uongozi nchini.
Rais Samia alikuwa Makamu wa Rais kwa miaka mitano mfululizo (Novemba 2015 hadi Machi 2021), katika serikali ya Dk. Magufuli, hadi mwanasiasa huyo alipofariki dunia, miezi minne baada ya kuapishwa kuendelea na muhula wa mwisho wa uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano.
“Dk. Magufuli aliweza kuamini mwanamke kuwa mgombea mwenza, nadhani alionekana wakati ule kama kigego (tatizo) hivi kwa kuchukua mwanamke kuwa mgomeba mwenza.
“Amefanya hivyo kwa maono, leo tusingekuwa na rais mwanamke, lazima tuendelee na yeye kumuweka katika historia ya kubadilisha sura ya uongozi wa taifa hili,” amesema Mongella.
Dk. Magufuli aliapishwa kumalizia uongozi wake katika Serikali ya Awamu ya tano tarehe 5 Novemba 2015, ambapo aliongoza kwa miaka mitano na kuingia ungwe nyingine ya 5 Novemba 2020 na kuongoza takribani miezi mitano, hadi alipofariki dunia.
Baada ya kufariki dunia Dk. Magufuli, Rais Samia aliapishwa kurithi mikoba yake.
Leave a comment