JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linamshikilia Latifa Bakari (33), mkazi wa Mabibo, kwa tuhuma za mauaji ya mtoto wa mdogo wake (2), aliyekabidhiwa kwa ajili ya kumlea. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa mapema leo, tarehe 12 Aprili 2022 na Kamanda wa Jeshi la Polisi wa kanda hiyo, ACP Jumanne Muliro.
Kamanda Muliro amesema, mtuhumiwa alifanya tukio hilo tarehe 5 Aprili mwaka huu, baada ya kumpiga kupita kiasi mtoto huyo, kisha tarehe 6 Aprili 2022, aliuchukua mwili wake kisha akaenda kuutupa maeneo ya River Side, Ubungo, jijini humo.
“Baada ya kubaini kuwa mtoto huyo amefariki baada ya kipigo, tarehe 12 Aprili 2022, mtuhumiwa aliuchukua mwili wa mtoto, kuukunja, kuuweka kwenye ndoo ya plastiki, kisha kuudumbukiza kwenye kiroba na kwenda kuutupa eneo la River Side UBUNGO,” amedai Kamanda Muliro.
Kamanda Muliro amesema, Jeshi la Polisi lilipata taarifa ya tukio hilo kutoka kwa majirani wa mtuhumiwa huyo, ambao waliitoa baada ya kutomuona mtoto.
“Baada ya majirani kutomuona mtoto huyo kama ambavyo si kawaida, walitoa taarifa Polisi, Polisi ilimuhoji kwa kina mtuhumiwa akakiri mauaji hayo na kwenda kuwaonesha Polisi mwili wa mtoto huyo ulipokuwa,” amedai Kamanda Muliro na kuongeza:
“Mwili huo umepelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa uchunguzi zaidi na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo baada ya mifumo ya kisheria kukamilika.”
Leave a comment