MKUU wa Mkoa wa Manyara, Makongoro Nyerere, amewataka wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wasiwe na wasiwasi kuhusu Makamu Mwenyekiti wa chama hicho Bara, Abdulrahman Kinana, akisema atatekeleza majukumu yake katika misingi iliyoachwa na viongozi waliopita. Anaripoti Mwandishi Wetu, Pwani … (endelea).
Makongoro ametoa kauli hiyo leo Jumamosi tarehe 9, Aprili 2022, akizungumza katika mdahalo wa kitaifa wa kuadhimisha miaka 100 ya kuzaliwa kwa Hayati Mwalimu Julius Nyerere, lililofanyika Pwani, mkoani Kibaha.
“Kaka yetu hivi sasa ni makamu mwenyekiti, wako wenye wasiwasi lakini nawaambia tusiwe na wasiwasi nchi yetu iko vizuri na huyu atatuongoza vizuri, kama alivyosema Mama (Rais Samia Suluhu Hassan), nchi itaongozwa katika misingi tuliyoachiwa na waasisi wetu,” amesema Makongoro.
Makongoro ametoa kauli hiyo akizungumzia hatua ya Mzee Philip Mangula, kung’atuka katika nafasi ya Umakamu Mwenyekiti wa CCM Bara, kisha nafasi yake ilichukuliwa na Kinana, aliyepitishwa kwa asilimia 100 kushika wadhifa huo na wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalumu wa chama hicho, uliofanyika jijini Dodoma, tarehe 1 Aprili 2022.
Amesema, kuna watu walihofia Mzee Mangula kung’atuka nafasi hiyo.
“Kinana sina nia mbaya, nasema tumepata mabadiliko kwenye uongozi wa juu, makamu mwenyekiti kuna mambo wanasema Mzee Mangula ameondoka, amekuja Kinana inakuwaje? Mimi nimegundua katika nchi hii siku zote hiyo ni wasiwasi wa bure,” amesema Makongoro.
Akimzungumzia baba yake, Hayati Nyerere, Makongoro amesema enzi za uhai wake alikuwa kiongozi mwenye maadili, ambaye alipenda kuenzi utu wa mwanadamu.
“Mwalimu Nyerere alikuwa muadilifu, mazungumzo yake yote yalikuwa yanazunguka jinsi gani nipate jinsi ya kutukuza kitu kinachoitwa uanadamu. Akikuona wewe una kona kona ambazo hazisaidii uanadamu, huwa hapendi kukaa karibu na wewe,” amesema Makongoro.
Leave a comment